Monday, May 13, 2013

WAHESHIMIWA MADIWANI, RAIA WASEMA HUDUMA ZA AFYA TUNDURU KIZUNGUMKUTI

Picha si ya tukio halisi  siku ilipotumwa habari na Mwandishi




Na Nathan Mtega,Tunduru
BAADHI ya wananchi na Madiwani Katika halmashauri ya Wilaya ya Tunduru mkoani Ruvuma wamelalamikia uduni wa huduma za afya zinazotolewa katika hospitali yao ya serikali, Vituo vya afya  na zahanati zilizopo wilayani humo.
Wakizungumza na mwandishi wetu kwa nyakati tofauti wananchi na baadhi ya madiwani walisema kuwa Pamoja na uduni wa huduma hizo za afya  pia kumekuwepo na uchakavu wa miundo mbinu ya chumba cha Kupasulia wagonjwa  katika hospitali ya wilaya.
Aidha, mazingira mabovu ya kutolea huduma hizo muhimu katika vituo vya afya na zahanati inasababisha wananchi kutokupata huduma ya afya ipasavyo kadri ya sera ya afya inavyojieleza.
Kero hizo, pia zilibainishwa na diwani wa  Kata ya Namasakata Zuhura Maftari, ambaye alilalamikia uchakavu na udogo wa majengo ya kujifungulia akina mama katika Hospitali ya Serikali ya Wilaya ya Tunduru huku kukiwa na majengo mapya yakiwa hayatumiki kwa sababu yanangojea kufunguliwa na viongozi wa ngazi za juu ndipo yaanze kutumika
Mhe. Mafutari, alisema kufuatia hali hiyo wanawake wanaokwenda kujifungua wamekuwa wakilala katika kitanda kimoja zaidi ya mgonjwa mmoja.
“hali  ni hatari kwao kwa sababu upo uwezekano mkubwa wa kuambukizana maradhi,” alisema na kuiomba serikali kupitia Wizara ya afya na Ustawi wa jamii kuona umuhimu wa kuruhusu majengo mapya yaliyopo kuanza kutumika badaka ya kusubiri mpaka yafunguliwe na viongozi wakati wananchi wanazidi kuteseka kwa kukosa huduma stahili.
Akizungumzia hali hiyo, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya hiyo, Robert Nehatta, pamoja na kukiri kuwepo kwa kero hizo na nyingine nyingi alisema  halmashauri ipo katika harakati za kuhakikisha kuwa inafanya marekebisho ya haraka katika maeneo yote ya kutolea huduma pamoja na kuruhusu majengo hayo mapya yaweze kuanza kutumika.

No comments:

Post a Comment