Thursday, May 23, 2013

LWAKATARE KUTWISHWA TENA ZIGO LA UGAIDI?

Mhe. Wilfred Lwakatare
 
MKURUGENZI wa Mashitaka (DPP) nchini, Dk Eliezer Feleshi amewasilisha ombi katika Mahakama ya Rufani nchini, akiomba mahakama hiyo itengue uamuzi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Dar es Salaam, wa Mei 8 mwaka huu, uliotolewa na Jaji Kaduri ambao ulimfutia jumla ya mashitaka matatu ya ugaidi Mkurugenzi wa Ulinzi na Usalama wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Wilfred Lwakatare na mwenziye Ludovick Joseph.

Dk Feleshi aliwasilisha ombi hilo juzi jioni kwa njia ya maandishi ambapo aliiomba mahakama hiyo ya juu kabisa nchini, iitishe mwenendo wa shauri lilotolewa uamuzi huo na Jaji Kaduri, na ipitie upya na iufute uamuzi huo kwa sababu una makosa kisheria.

Dk Feleshi anadai sababu kuwasilisha ombi lao ni kwa kuwa Lwakatare hakuwahi kuomba Mahakama  Kuu imfutie mashitaka kama jaji Kaduri alivyofikia uamuzi huo, bali Lwakatare aliiomba Mahakama Kuu iitishe majadala ya kesi ya msingi iliyofunguliwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu tarehe 18 na 20 Machi 2013, dhidi yake na kisha iyapitie, kwa kuamini kuwa DPP alitumia madaraka yake vibaya kwa kumfutia kesi Na.37 na kisha Machi 20, kumfungulia tena kesi Lwakatare kwa makosa yayo hayo.

“Kwa kuwa ofisi ya DPP ipo kwa ajili ya kusimamia utawala wa sheria, haujaridhishwa na uamuzi wa Mahakama Kuu uliomfutia mashitaka yale matatu Lwakatare, hivyo tunaiomba Mahakama hii iitishe mwenendo wa kesi ulioamuriwa na Mahakama Kuu uupitie, kwani tunaamini kisheria Jaji alikosea kutoa uamuzi ule kwani Lwakatare hakuwa ameomba afutiwe mashitaka yanayomkabili,”alidai Dk Feleshi.

Hadi jana mchana, uongozi wa Mahakama ya Rufaa ulikuwa bado haujapangia majaji wa kusikiliza ombi hilo.

---
Ni sehemu ya taarifa iliyoandikwa na Happiness Katabazi na kuchapishwa kwenye gazeti la TanzaniaDaima.


Source: http://www.wavuti.com/#ixzz2U6AFrpdm

No comments:

Post a Comment