Wednesday, May 29, 2013

UHABA WA VYOO SHULENI KIKWAZO KINGINE KATIKA KUBORESHA ELIMU

Mkuu wa Shule ya Sekondari Londoni, Mwl. Chris Mwageni (katikati) akihojiwa na waandishi wa habari wa Jogoo FM Aden Mbele aliyeshika kinasa sauti na Tamimu Adamu ( kushoto) wakifuatilia nini kiini cha tatizo la vyoo katika shule za msingi, Sekondari vyuo na pengine hata sehemu za kazi. Mahojiano hayo yalifanyika Ofisi za Magazeti Vijijini Kanda ya Kusini, Uwaqnja wa sabasaba-Matarawe Songea jana.
Na Mwandishi wetu.
UHABA wa vyoo katika shule za msingi, sekondari na hata vyuo mbalimbali hapa nchini ni kikwazo kingine cha kuboresha mazingira ya kujifunza na kufundishia.
Hayo yamesemwa na Mwenyekiti wa Marafiki wa Elimu Songea, Bw. Juma Nyumayo, wakati akihojiwa na Redio Jogoo FM ya mkoani Ruvuma.
Bw. Nyumayo amesema takwimu zinaonyesha kuna uhaba mkubwa wa choo shuleni na wakati huohuo katika majengo yaliyokamilika katika Shule za sekondari au vyuo miundombinu yake kuharibiwa kwa makusudi au kutokuwa na elimu ya kuvitumia vyoo hivyo.
"Mfano kwenye baadhi ya  shule au vyuo vya elimu ya juu wanakotumia vyoo vya kisasa miundombinu yake imeharibiwa na kusababisha adha kubwa," amefafanua kuwa hiyo ni kwasababu ya kukosa mafunzo yanayozingatiwa na watumiaji wa vyoo hivyo.
Akizungumzia shule za msingi ambako kuna baadhi ya Shule kutokuwa na choo kabisa au walimu na wanafunzi kutumia choo kimoja, Mwenyekiti Nyumayo amesema hilo ni tatizo linalowakabili wadau wa elimu kutohakikisha ujenzi kulingana na sera na kuweka choo kama kitu kidogo katika shule.
"Hapa ni uzoefu tunaoupata kuwa hata baadhi ya nyumba katika jamii zetu hazina vyoo, hivyo jamii inaona hata shule hazina umuhimu wa kujengewa choo," alisema.
Alifafanua kuwa hata shule za vyoo, vyoo vyake ni vichafu au vimejaa na wadau wa elimu hawachukuwi hatua.
"Sisi kama marafiki wa elimu mkoani hapa tunaomba kuangalia upya namna ya kuboresha vyoo na view safi muda wote ili kupafanya shuleni mahali bora pa kuishi walimu na wanafunzi, kuliko ilivyosasa," alisema Bw. Nyumayo.
Naye Mkuu wa Shule ya Sekondari ya Londoni yenye kidato cha I-VI,  Mwl. Christopher Mwageni, amesema yeye anaishukuru serikali na jumuia ya shule yake kwa kuvijenga vyoo vya kutosha katika shule hiyo.
Mwl. Mwageni alisema kutokana na changamoto ya choo wanafunzi wake hupewa mafunzo ya namna ya kutumia choo na maarifa hayo kuhamishia nyumbani kwao.
Amesema walimu na wanafunzi wanaotumia choo kimoja huathirika kisaikolojia na kuharibu mfumo mzima wa kufunisha na kujifunza.
"Mwalimu anayelazimika kuvizia kwenda choo cha wanafunzi na wanafunzi wanaovizia kwenda choo anachotumia mwalimu huathirika kisaikolojia," alisisitiza Mwl. Mwageni.
Kwaujumla wadau hao wote wawili wameomba serikali za mitaa na vijiji kusimamia ujenzi wa vyoo katika shule zao.
Mwisho

No comments:

Post a Comment