Saturday, July 13, 2013

RUVUMA WAFANYA MAANDALIZI YA KUMPOKEA WAZIRI MKUU MIZENGO PINDA

 Hivi ndivyo mji unavyoonekana leo katika baadhi ya barabara za Manispaa ya Songea
 Gari likisukumwa baada ya kukaa muda mrefu katika garage bubu iliyopo mitaa ya Buhemba
 Mji safi
Hapa ni mtaa wa Dilux magari yakiwa yamepangwa katika utaratibu mzuri
Mji unawake
Wafanya biashara wa matunda katika eneo hili la Dilux wameondolewa kutokana na ujio wa Waziri Mkuu Mizengo Pinda mkoari Ruvuma
Dereva Yebo wakiwa katika vituo vyao kwa utaratibu mzuri
Gari la Manspaa likiwa kazini maeneo ya bombambili huku wafanya kazi wakiwa wanazoa na njia hii atapita akiwa anaelekea kukagua miradi na kuweka jiwe la msingi katika baadhi ya maeneo
 Hii ni sehemu moja wapo iliyobomolewa vibanda ikiwa ni  kuweka mji safi
Hapa ni maeneo ya Bombambili upakaji wa rangi alama za barabarani ukiendelea siku ya leo kabla ya Waziri mkuu kutua Ruvuma hapo kesho

Habari kwa hisani ya www.demashonews.blogspot.com

Friday, July 12, 2013

MAGAZETI YA LEO IJUMAAA 12/7/2013 NA YALIYOCHOMOZA


.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.

MAAFISA WAHALMASHAURI YA WILAYA YA MBINGA WATEMBELEA TUJIFUNZE

Maafisa wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga, (Kutoka kushoto) Mweka hazina Bw. Stephen Sindagulu, Mhasibu,  Bw. David Mkande na Mhasibu, Bw Joseph Mazito. na hapo chini pia leo katika ofisi ya Tujifunze Songea



MAAFISA wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga, wmetembelea Kituo cha Uchapaji (Rural Press Songea) ambacho ni Kituo cha Magazeti Vijijini Kanda ya Kusini yenye makao makuu yake Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma, kwa lengo la kujifunza na kuimarisha uhusiano wa kituo hicho na Halmashauri ya wilaya ya Mbinga.
Kiongozi wa Ziara hiyo fupi ya Maofisa watatu, Mweka Hazina wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga, Bw. Stephen Sindagulu, amesema imekuwa ya mafanikio makakubwa kwani wameweza kujionea mahali kazi zao zinapochapwa na kuzungumza na uongozi wake na kuona mitambo iliyopo kiwandani hapo.

Akiwa ameongozana na Wahasibu wawili toka Ofisi yake, Bw. David Mkande na Bw. Joseph Mazito, Mweka Hazina huyo, Bw. Sindagulu, alipata kuziona baadhi ya mashine na kazi zinazofanywa pia kukagua aina mbalimbali ya karatasi kulingana na mahitaji ya wateja kuzihitaji kuchapiwa kazi zao.
 
 Kazi zinazochapwa na Kituo hicho cha Magazeti vijijini Kanda ya Kusini, licha ya kuchapisha Gazeti la Kanda ya Kusini, Tujifunze, huchapa pia   nyaraka mbalimbali za kiserikali za Sekta ya Elimu katika kunyanyua ubora  wa taaluma katika shule za msingi, sekondari na vyuo pia Idara nyingine kama Afya, Kilimo, Utawala na nyinginezo.

Huchapisha pia vitu  mbalimbali  vya watu binafsi na serikali kwa maagizo wayatakayo ikiwa ni pamoja na vitabu vya risiti, tiketi za kusafiria,  stakabadhi za malipo mbalimbali ikiwa ni pampja na fomu za malipo kama TFN 4 na 5.
Mhariri wa Tujifunze, Bw Christian Sikapundwa, ameupongeza uongozi wa halmashauri ya Mbinga kwa kutembelea Kituo chake na kusema ni mfano wa kuigwa na Halmashauri nyingine katika Kanda ya Kusini.
"Ziara yenu fupi ya kuona kazi zenu huchapwa wapi na kwa ubora gani imepokelewa vizuri, na tunaamini wengine watafuata nyayo zenu,' alisema Bw. Sikapundwa.

Alisema Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga inaendeleza uhusiano mwema uliojengeka na Kituo chake toka Enzi ya Mweka hazina wa halmashauri hiyo ambaye sasa amepanda hadi kuwa Katibu Mkuu mmojawapo katika Serikali ya awamu ya Nne , Bw. Rashid Katanga.


 

Thursday, July 11, 2013

ENEO LA MSHANGANO MANISPAA YA SONGEA LAPANDA THAMANI


Moja ya Barabara kubwa zinazochongwa katika mitaa eneo la Mshangano ikiwa ni utekelezaji wa Mradi wa Upimaji wa Viwanja 18,000 unaofanywa na Kampuni Binafsi ya Ardhi Plan Ltd ya Dar es Salaam chini ya Mkurugenzi wake Bw. Gombo Simanditto, ili kurasmisha makazi na kuwafanya wananchi wajenge nyumba bora na kulinda usafi wa mazingira.

 
 

Hii ni moja ya barabara iliyochongwa katika eneo hilo pia, nyumba zinazoonekana kwa mbali ni eneo la Msamala kwa Gassa Manispaa ya Songea.

 

Baadhi ya  vibarua wa Kampuni ya Ardhi Plan Ltd ya Dar es Salaam wakipanga "Mawe yenye namba" Beacons tayari kwa kupanda katika viwanja vilivyopimwa rasmi mkawaajili ya makazi bora ya watu huko eneo la Misufini Mtaa wa Namanyigu ambapo zoezi hilo linakwenda sambamba na uchongaji barabara za mitaa leo.


Mheshimiwa Diwani wa Kata ya Mshangano Manispaa ya Songea, Faustine Mhagama akionyesha njia za mwanzo kuchongwa ili kuimarisha miundombinu ya barabara  Kata ya Mshangano, Songea.


MRADI waKurasmisha makazi na kupima Viwanja 18,000 katika mashamba na baadhi ya nyumba ambazo zilijengwa kiholela maeneo ya Mitaa ya Namanyigu, Mshangano na Muumbezi Kata ya Mshangano manispaa ya Songea umekuwa wa mafanikio makubwa na kuleta sura mpya ya kata hiyo.

Mafanikio hayo ni pamoja na watu wa kawaida, viongozi na wamiliki wa maeneo kutambua umuhimu wa upimaji baada ya eneo hilo sasa viwanja vyake kupanda thamani ghafla na kuwa kimbilio la watu wengi kutaka kujenga.

Licha ya watui wengi kukimbilia eneo la Kata ya Mshangano, mradi huo umeboresha kwa kiasi kikubwa miundombinu ya barabara ambazo hivi sasa zinaendelea kuchongwa katika Mtaa wa namanyigu na kuwafanya watu waione ramani halisi iliyochorwa katika karatasi ardhini.

Watu kadhaa waliohojiwa wameufurahia mpango huo na kusema kitendo cha kampuni ya Ardhi Plan Ltd toka Dar es Salaam kutekeleza ahadi yake kama mkataba ulivyokuwa na kuzichoinga barabara zao hawaamini na kwamba umekuwa ukombozi mkubwa.
Bw Salum Muhagama mkazi wa namanyigu, alisema hajawahi kuona kuchongwa barabara katika maeneo ya makazi kama ilivyokuwa katika mradi huo.
"huu ni ukombozi mkubwa , tangu nianze kuishi katika mji huu wa Songea sijawahi kuona utaratibu wa kuchonga barabara kama hizi," alisema Mhagama na kutolea mifano ya maeneo ya making'inda, Mkuzo, Msamala kwa gasa na hata mateka hawakuwahi kuzichonga barabara.

Viwanja hivyo 18,000 vilivyopimwa na kampuni Binafsi ya Ardhi Plan Ltd ya dar es Salaam ndiyo mradi wa kwanza wa aina yake hapa mkoani Ruvuma kushirikisha wananchi ambao waliiajiri kampuni Binafsi kupima viwanja na kuwa mfano wa kuigwa.
Kampuni hiyo ilipima viwanja vingi kwa wakati kurasmisha makazi bila kuwaondoa wenye ardhi/mashamba yao kwa kuwalipa fidia zisizokwenda na bei ya soko kama walivyofanya halamashauri ya manispaa ya Songea katika eneo la namanyigu katika Mradi uliokula Shilingi Milioni 80 bila kuchonga barabara hata moja.
Mradi huo ambao umeleta maendeleo ya makubwa na ya haraka katani Mshangano uliwhi kuleta sintofahamu kiasi kwamba Diwani wa kata hiyo Bw Faustine Muhagama aliwekwa ndani kituo cha polisi cha kati Mjini Songea kwa kupigia debe mradi huo ambao ulipata upinzani mkubwa.

Mafanikio ya Mradi huo yaliyoletwa kwa pamoja kati ya Wananchi wa Mitaaa Mitatu ya Mitendewawa, Mshangano na Namanyigu  kata ya Mshangano yamekuwa mfano bora wa utawala bora katika kudhibiti maliasili ardhi iliyomkuwa ikimilikiwa toka enzi za mababu kwa na kukubalika na Sera ya maendeleo ya Ardhi hapa nchini.


Wednesday, July 10, 2013

RAIS KIKWETE NA MIAKA 50 YA JKT




HOTUBA YA RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, MHE. DKT. JAKAYA MRISHO KIKWETE KATIKA KILELE CHA SHEREHE ZA KUADHIMISHA MIAKA 50 YA JESHI LA KUJENGA TAIFA UWANJA WA UHURU, 10 JULAI, 2013, DAR ES SALAAM

Mheshimi wa Shamsi Vuai Nahodha (Mb), Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa;
Mheshimiwa Gril Haskel, Balozi wa Israel;
Meja Jenerali Raphael Muhuga,Mkuu wa Jeshi la Kujenga Taifa,
Makamanda, Wapiganaji na Vijana;
Wageni Waalikwa;
Ndugu Wananchi;
Mabibi na Mabwana;
Pongezi
Nakushukuru sana Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Mheshimiwa Shamsi Vuai Nahodha na Mkuu wa Jeshi la Kujenga Taifa (JKT), Meja Jenerali Raphael Muhuga kwa kunishirikisha kwenye sherehe za maadhimisho ya miaka 50 ya uhai wa Jeshi la Kujenga Taifa.  Nawapongeza sana kwa maandalizi mazuri ya sherehe hizi ambazo hakika zimefana sana.  Gwaride lilikuwa zuri na tumeburudika vya kutosha kutoka vikundi vya ngoma, ngonjera na nyimbo. 
Kwa niaba yangu, ya Serikali na ya Watanzania wote nawapongeza kwa dhati Maafisa Wakuu, Maafisa Wadogo, wapiganaji na vijana wa JKT popote pale walipo kwa kusherehekea Jubilei ya Dhahabu ya uhai wa JKT.  Mnastahili kuwa na furaha na kusherehekea kama tulivyoshuhudia sote. 



Historia ya JKT
Ndugu Wananchi;
Miaka 50 iliyopita, tarehe kama ya leo, yaani tarehe 10 Julai, 1963 Jeshi la Kujenga Taifa lilianzishwa rasmi.  Huu ulikuwa ni utekelezaji wa Azimio la Kikao cha Baraza la Mawaziri kilichofanyika tarehe 19 Aprili, 1963 chini ya uongozi wa Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, aliyekuwa Rais wa Jamhuri ya Tanganyika. Wazo la kuanzishwa kwa JKT lilitokana na mapendekezo ya busara ya Mkutano Mkuu wa Umoja wa Vijana wa Chama cha Tanganyika African National Union (TANU Youth League), uliofanyika mkoani Tabora mwaka 1958.  Wazo hili lilitolewa na Katibu Mkuu wa TANU Youth League wakati ule Ndugu Joseph Nyerere ambaye sasa ni marehemu.  Lengo kuu la kutaka kuundwa kwa JKT lilikuwa ni kuwandaa vijana kuwa raia wema, wawe na moyo wa uzalendo, na wawe tayari kulitumikia taifa lao kwa nguvu na uwezo wao wote. 
Ndugu Wananchi;
            Jeshi la Kujenga Taifa lilianza na Vijana 11 kutoka Wilaya 11 nchini.  Hao ndio walikuwa wa kwanza kupata mafunzo katika Kambi ya JKT Mgulani, Jijini Dar es Salaam.  Vijana hao walikuwa ni Makatibu wa Umoja wa Vijana wa TANU na wengine walimu.  Niruhusuni niwatambue watu hao kuwa ni Bi Zainabu Kiango, Bw. Sebastian Chale, Bw. Peter Lwegarulira, Bw. Rupho Kamba, Bw. Hashim Ngaliwason, Bw. John Ndimugangwo, Bw. Said Desai, Bw. Dismas Msilu (Brigedia Mstaafu), Bw. Athumani Msonge (Brigedia Jenerali Mstaafu), Bw. Reginald Mitande na Bw. Eslei Mwakyambiki. 
Kati ya hao 11, walio hai ni Bi Zainabu Kiango na Brig. Jenerali Dismass Msillu ambao wapo nasi siku ya leo.  Waliosalia wameshatangulia mbele ya haki.  Mwenyezi Mungu awarehemu.  Kundi la pili liliwajumuisha Bi. M. Mhando, Bw. E. Simkone, Bw. Mwanimlele (Asst Master) Bw. AA Moyo (Asst Master) ambao walijiunga na kupata mafunzo ya uongozi. 
Sheria Iliyoanzisha JKT
Ndugu Wananchi;
Mwaka 1964, Bunge lilitunga Sheria ya Kuanzisha JKT iliyoupa nguvu ya kisheria uamuzi wa mwaka 1963 wa Baraza la Mawaziri wa kuanzishwa kwa Jeshi hilo.  Kwa mujibu wa Sheria ile, kujiunga na JKT ilikuwa jambo la kujitolea kwa mapenzi ya mtu. Lakini mwaka 1966, Sheria hiyo ilifanyiwa marekebisho na kuanzisha utaratibu wa kujiunga na JKT kwa mujibu wa Sheria.
  Utaratibu huu uliwahusu vijana waliohitimu vyuo vikuu, vyuo vya elimu ya juu, kidato cha sita na waliomaliza kidato cha nne ambao wamepata mafunzo kwenye vyuo vya taaluma mbalimbali kama vile ualimu, uganga, uuguzi na kadhalika.    Mkurugenzi wa JKT aliwezeshwa kisheria kuwaita vijana hao kujiunga na JKT.  Mwezi Julai 1967, kikundi cha kwanza cha vijana wasomi 64 kilijiunga na JKT katika Operesheni Azimio. 
            Katika kuunga mkono uamuzi wa Serikali kuhusu kuanzishwa kwa Jeshi la Kujenga Taifa, viongozi na wasomi wengine waliohitimu zamani waliamua kujiunga na mafunzo ya JKT.  Mwezi Januari, 1968, kwa mfano, aliyekuwa Makamu wa Pili wa Rais, Mheshimiwa Rashid Kawawa, aliyekuwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais, Mheshimiwa Aboud Jumbe, aliyekuwa Spika wa Bunge Chifu Adam Sapi Mkwawa pamoja na baadhi ya Wabunge na viongozi mbalimbali wa Chama na Serikali walijiunga na mafunzo ya Jeshi la Kujenga Taifa.  Wote walikuwa katika kambi ya Ruvu ambapo walipatiwa mafunzo ya uongozi.
Ndugu Wananchi;
Mwaka 1975 JKT iliunganishwa na Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania na hivyo kuwa sehemu kamili ya JWTZ.  Kuanzia wakati ule, Maafisa na Askari wa JKT wakawa ni wa JWTZ na kutambulika kwa vyeo vya JWTZ.  Jeshi la Kujenga Taifa liliendelea na majukumu yake ya kutoa mafunzo kwa vijana wa kujitolea na wa mujibu wa sheria.  Hata hivyo, mambo mawili ya msingi yalisisitizwa au kuongezwa katika majukumu ya JKT.  Kwanza kwamba, kuwa Divisheni ya Uzalishaji ya JWTZ yenye dhamana ya kulipatia Jeshi mahitaji yake ya chakula, mavazi na mengineyo.  Pili, kwamba JKT ndipo mahali pa kutolea mafunzo ya awali ya kijeshi na kwamba JWTZ itaajiri kutokana na wanaohitimu JKT. 
Katika dhamira ya kutimiza wajibu wa kwanza kwa ufanisi, mwaka 1982 Shirika la Uzalishaji Mali la JKT (SUMAJKT) liliundwa.   Shabaha kuu ilikuwa ni kuwa na chombo madhubuti cha kupanga, kusimamia, kuratibu na kutekeleza majukumu ya uzalishaji mali na kiuchumi katika JKT kazi ambayo shirika linaendelea kuifanya hadi sasa.
Kusitishwa kwa Mafunzo ya JKT
Ndugu Wananchi
Tunapoangalia nyuma, katika historia ya miaka 50 ya kuzaliwa na uhai wa JKT tunaona wazi kuwa yamepatikana mafanikio makubwa.  Tena ni mafanikio ya kutia moyo na kujivunia.  Ninaposema hivyo, napenda nisieleweke vibaya kuwa sitambui ukweli kwamba kulikuwepo vipindi vigumu vyenye changamoto za namna mbalimbali.  Zilikuwepo changamoto kubwa na ndogo na zilizokuwa ngumu na nyepesi kuzipatia ufumbuzi.  Aidha, natambua kuwa bado zipo changamoto kadhaa tunazoendelea kukabiliana nazo.  Jambo la msingi na la faraja ni kwamba pamoja na changamoto hii tumefanikiwa sana.
Ndugu Wananchi;
Kwa upande wa mafunzo kwa vijana, kwa mfano, zaidi ya vijana 305,625 wamepitia JKT na kupatiwa mafunzo ya kijeshi na ya stadi mbalimbali za maisha katika fani na nyanja mbalimbali.  Tangu mwaka 1963 mpaka sasa yameshapita makundi (kwa jina maarufu Operesheni) 102. 
Bahati mbaya kwa sababu ya hali mbaya ya uchumi iliyoikabili nchi yetu kuanzia nusu ya pili ya miaka ya 1970 na kuwa mbaya zaidi miaka ya 1980 na mwanzoni mwa 1990, hali ya utoaji wa mafunzo kwa vijana katika JKT iliathirika sana.  Upatikanaji wa huduma na mahitaji kwa ajili ya mafunzo na kuendesha kambi na JKT kwa jumla ukawa mgumu.
Pengine ni vyema nikaeleza kuwa kupanda sana kwa bei ya mafuta duniani, kuanguka kwa bei za mazao yetu tunayouza nje na gharama kubwa ya vita dhidi ya Idi Amin wa Uganda ndivyo vilivyosababisha uchumi wa nchi yetu kutetereka.   Hali hii ilipunguza sana uwezo wa Serikali kutimiza majukumu yake ya msingi katika sekta, karibu zote nchini.
Ndugu Wananchi;
Kwa sababu hiyo, kwa upande wa JKT mwaka 1993, Serikali ililazimika kusimamisha mafunzo kwa vijana wa kujitolea na mwaka 1994 ilifanyika hivyo kwa vijana wa mujibu wa Sheria.  Kwa kweli baada ya mwaka 1994 shughuli za msingi za JKT zilidorora sana na kubakiza za kulinda kambi na zile Shirika la Uchumi (SUMAJKT).  Hata hizo nazo hazikuwa zinafanyika kwa kiwango kikubwa wala hazikuwa kwa ufanisi mkubwa kwa sababu ya kutokupata fedha za kutosha kutoka Serikalini.  Fedha za uendeshaji wa shughuli zake zilikuwa kidogo.
Ndugu Wananchi;
            Kuifufua JKT ilikuwa ni moja ya mambo niliyoyapa kipaumbele cha juu nilichojiwekea katika mipango ya kazi baada ya kupewa heshima kubwa ya kuliongoza taifa letu Desemba 21, 2005.  Mtakumbuka kuwa katika hotuba yangu ya kuzindua Bunge tarehe 30 Desemba, 2005, nilipozungumzia kufanya kila tuwezalo kujenga moyo wa utaifa na uzalendo miongoni mwa vijana, nilikuwa nazungumzia kufufua na kuimarisha Jeshi la Kujenga Taifa pamoja na kuwepo kwa shule za kitaifa hasa za sekondari.
Ni ukweli ulio wazi kwamba JKT imefanya kazi kubwa na nzuri ya kujenga moyo wa utaifa na uzalendo miongoni mwa vijana waliopitia Jeshi hilo.  Hapa ni mahali ambapo vijana wa rangi zote, makabila yote, dini zote hukutana, kuishi pamoja na kufanya mafunzo na kazi kama ndugu wa nchi moja.  Hakuna chombo chochote cha malezi ya vijana kilichoizidi JKT katika kazi hiyo.  Kwangu mimi na wenzangu katika Serikali ninayoiongoza kufufua mafunzo ya vijana wa kujitolea na mujibu wa sheria lilikuwa suala kubwa na muhimu sana kulitekeleza.
Ndugu Wananchi;
            Bahati nzuri sikuwa peke yangu mwenye fikira na matamanio hayo.  Watu wengi ndani ya Serikali, nje ya Serikali na miongoni mwa raia na Bungeni walikuwa wanaunga mkono mawazo hayo.  Sababu kubwa ni kuwa athari za kusimamishwa mafunzo ya JKT ziliwagusa wengi na ndiyo maana kumekuwepo na madai ya kutaka mafunzo yarudishwe.
Kule Bungeni kauli yangu kuhusu JKT iligeuka kuwa deni kubwa kwangu na kwa Serikali.  Madai ya kutaka Serikali irejeshe mafunzo ya JKT kwa mujibu wa Sheria yalikuwa yanajitokeza mara kwa mara na mwangi wake ulikuwa unaongezeka ukali kila mwaka.  Nafurahi kwamba hatimaye tarehe 26 Machi, 2013 tulifanikiwa kutimiza dhamira na ahadi yetu nilipozindua kuanza upya kwa mafunzo hayo katika kambi ya Ruvu.  Kundi la kwanza limemaliza mafunzo yake na la pili limeshafika katika makambi na tayari wameanza mafunzo.
            Kama ilivyokuwa mwaka 1964 JKT ilipoanza, na mwaka 1968 baada ya mafunzo ya mujibu wa Sheria kuanzishwa, viongozi wa kitaifa waliongoza kwa mfano; safari hii Wabunge wetu alionesha.  Mwaka huu Wabunge 22 wamefanya na kumaliza mafunzo ya uongozi.  Baadhi yao wako nasi siku ya leo.  Niruhusuni nirudie kutoa pongezi zangu za dhati kwao kwa kuwa viongozi wa mfano.


Ndugu Wananchi;
            Taarifa nilizonazo ni kuwa wamefanya na kumaliza mafunzo yao vizuri.  Walikuwa na nidhamu nzuri, utii na moyo wa kujituma.  Wamemaliza wakiwa ni askari wakakamavu na wenye mtazamo mpya na bora zaidi kuhusu masuala ya utaifa, uzalendo na mustakabali wa taifa letu na watu wake. 
Ndugu Wananchi;
            Kwa upande wa shughuli za kiuchumi zinazofanywa na JKT tuliazimia kuwa, tutafanya kila tuwezalo kuimarisha SUMAJKT.  Tumefanya mambo kadhaa kwa ajili hiyo na tumekuwa tunapata mafanikio ingawaje bado tunayo safari ndefu ya kulijenga shirika hili mpaka liwe bora kwa shughuli lizifanyazo.  Naamini tutafika pale tunapopatarajia. 
 Tuliamua kutoa upendeleo maalum kwa JKT kwa kutoa shughuli na miradi kadhaa ya Serikali waitekeleze wao.  Kwa mfano, ujenzi wa nyumba na majengo kadhaa ya Serikali pamoja na ujenzi wa barabara, mabwawa ya maji na miradi ya kilimo cha umwagiliaji na kadhalika.  Tumewapa JKT kazi ya kuzalisha mbegu bora kwa wakulima.  Vile vile, Serikali imechukua mkopo wa dola za Marekani milioni 40 kutoka Serikali ya India uliotumika kununua matrekta 1,846 kutoka Serikali ya India na kuipa SUMAJKT kuuza kwa wakulima kama biashara yao. 
Hivi sasa mchakato unaandaliwa wa kupata mkopo mwingine wa dola za Marekani milioni 92 kwa ajili hiyo.  Tumefanya yote hayo kwa makusudi mazima ya kuliwezesha Jeshi la Kujenga Taifa kuwa na shirika lililoimara na linalotekeleza kwa ufanisi majukumu yake.  Halikadhalika itawezesha JKT kudumisha sifa yake nzuri katika kilimo, ufugaji, uvuvi na ujenzi.
Ndugu Wananchi;
            Napenda kuchukua nafasi hii, kuwashukuru kwa dhati ya moyo wangu, Wakuu wa JKT kumi, waliotangulia pamoja na Meja Jenerali Muhuga aliyepo sasa.  Tunawapongeza kwa utumishi wao uliotukuka na moyo wao wa upendo kwa nchi yetu na watu wake.   Mafanikio haya tunayojivunia leo yametokana na juhudi kubwa za viongozi hawa wakishirikiana na maafisa, askari na wafanyakazi raia katika kubuni na kusimamia utekelezaji wa shughuli za JKT. 
Mimi na Watanzania wenzangu wote hatuna neno lingine zuri la kuwaonesha upendo wetu na shukrani zetu zaidi ya kusema asanteni sana.  Tunatambua na kuthamini mchango wenu.  Tutauenzi daima.
Changamoto na Dira
Mheshimiwa Waziri;
        Pamoja na mafanikio ya kutia moyo, naelewa kuwa bado safari iliyo mbele yetu ni ndefu na imejawa na changamoto nyingi ambazo hatuna budi kuzipatia majawabu.  Miongoni mwa changamoto hizo ni pamoja na uhaba wa makazi ya maafisa na askari, upungufu wa wataalamu katika miradi mbalimbali, upungufu wa vitendea kazi na vyombo vya usafiri.  Baadhi ya makambi hayana miundombinu mizuri ya kutoa kwa uhakika huduma muhimu kama vile maji, umeme na kadhalika.
Napenda kuwaahidi kuwa Serikali itaendelea kushirikiana na JKT katika kutafuta njia mbalimbali za kuzipatia ufumbuzi changamoto hizo.  Tutaendelea kuongeza bajeti ya JKT kila mwaka na kuidhamini SUMAJKT ipate mikopo ya kutekeleza miradi yake na shughuli zake.  Tutaendelea kutoa upendeleo kwa Jeshi na JKT katika kutekeleza baadhi ya miradi ya Serikali.  Hata hivyo, nawaomba mzingatie ubora wa kazi muifanyayo ili kulinda heshima ya JKT na  kutulinda sisi tunaoamua kuwapa upendeleo.
Ndugu Wananchi;
Tunafanya haya kwa dhamira moja kubwa ya kutaka kulifufua Jeshi la Kujenga Taifa na kulifikisha mahali panapostahili na kuwa chombo madhubuti cha kutumainiwa na taifa.  Nataka JKT liwe Jeshi la kisasa zaidi, linaloenda na wakati na kutimiza majukumu yake kwa ufanisi wa hali ya juu.  Tunapenda mafunzo yanayotolewa kwa vijana wanaojiunga na JKT yaendeshwe vizuri.  Tunataka JKT itoe wazalendo wa kweli, wanaothamini utaifa, umoja na mshikamano wa Watanzania.  Vijana wanaopenda kufanya kazi kwa moyo wa kujituma na kujitolea.  Tunataka JKT izalishe askari walio hodari na wanaoweza kulinda nchi yao kwa ujasiri mkubwa.  Aidha, wanapoajiriwa na vyombo vya ulinzi na usalama na kwingineko, idhihirishe wazi kuwa vijana waliopitia JKT ni bora.  Ni watu walioiva, wa kuaminika na kutumainiwa. 
Hali kadhalika, kwa wale wanaorudi uraiani kufanya shughuli nyingine wawe ni watu waliokamilika na wenye uwezo wa kusimama wenyewe na kuendesha maisha yao.  Kinachotakiwa ni kuwepo kwa utaratibu mzuri kuwasaidia wanaojiajiri waweze kuanzisha shughuli za kuwaingizia mapato kwa kutumia ujuzi na maarifa waliyoyapata.  Namna ya kuwawezesha vijana wanaomaliza JKT waanze maisha ya kujitegemea ni jambo ambalo hatuna budi kulitafakari.  Lakini leteni mapendekezo yenu tuone namna ya kuyatekeleza.
Ndugu Wananchi;
Mpaka sasa bado JKT haijafanikiwa ipasavyo kuwa divisheni ya uzalishaji ya JWTZ kama ilivyotarajiwa.  Bado haizalishi chakula cha kutosheleza mahitaji ya JWTZ.  Aidha, bado hawajaweza kutosheleza mahitaji mengine ya JWTZ kama vile mavazi na kadhalika.  Sasa wakati umefika wa kujipanga vizuri kutekeleza jukumu hilo.  JKT itumie sherehe hizi kufunga nadhiri ya kupanga na kuanza safari ya dhati ya kufanya hivyo.  Lakini, wasiishie hapo tu, JKT iweke nia ya kuzalisha ziada ya kuuza nchini na hata nje ya nchi.  Inawezekana, jipangeni vizuri ili mtimize wajibu wenu. 
Rai kwa Makamanda wa JKT
Ndugu Mkuu wa JKT, Makamanda, Maafisa na Askari;
        Ni jambo linalotia faraja kubwa kwamba sote tunatambua kuwa katika miaka 50 iliyopita Jeshi la Kujenga Taifa limepata mafanikio ya kutia moyo ingawaje safari ilikuwa na vikwazo mbalimbali.  Hata huko mbele muendako hatutegemei kuwa mambo yatakuwa rahisi, changamoto mbalimbali zitaendelea kujitokeza.  Hivyo basi, kinachohitajika ni kuendelea kuwa wabunifu kufanya kazi ya ziada, tena kwa bidii zaidi, maarifa na moyo wa kujituma na kujitolea.  Hizi ni sifa ambazo mnazo, hivyo naomba muendelee kuzidumisha na kuziendeleza.
 Endeleeni kuwa chuo mahiri cha kuwafunda vijana wetu wawe na moyo wa utaifa, uzalendo, kujituma na kupenda kufanya kazi.  Wawe raia wema na wawe tayari kutoa mchango stahiki katika kujenga taifa lao.  JKT inategemewa kuendelea kuwa kitovu cha shughuli za uzalishaji mali, mafunzo ya stadi za kazi na ujasiriamali kwa vijana wetu.  Endeleeni kuimarisha JKT.
  Nawaomba mtimize wajibu wenu huo kwa ukamilifu.  Msituangushe.  Nawaomba endeleeni kuwa na moyo wa kuchapa kazi, muwe  makini na waaminifu katika utendaji wenu wa kazi za kila siku.  Tafadhali zingatieni sana viapo vyenu vya utumishi jeshini kwa kila ngazi ya uongozi.  Muwe na nidhamu siku zote kama mwanajeshi anavyotakiwa kuwa.  Mkifanya hivyo, nina imani kuwa katika miaka michache ijayo JKT itapiga hatua kubwa ya maendeleo.  Taifa litanufaika sana.
Shukrani kwa Israel
Ndugu Wananchi;
Nitakuwa mwizi wa fadhila kama sitatambua na kuwashukuru marafiki zetu wa Israel.  Nchi ya Israel ndiyo iliyotupatia wakufunzi wa kwanza waliotusaidia katika kuanzisha Jeshi la Kujenga Taifa.  Aidha, walitoa mafunzo kwa viongozi wetu kadhaa waasisi wa JKT nchini Israel.  Serikali ya Israel imewakilishwa hapa leo na Balozi wake nchini Mheshimiwa Gril Haskel.  Naomba Balozi atufikishie salamu zetu nyingi za shukrani kwa Rais Shimon Peres, Waziri Mkuu Benjamin Netanyahu na watu wote wa Israel kwa mchango wao muhimu walioutoa katika kuanzisha na kujenga Jeshi la Kujenga Taifa.  Hatasahau kamwe.

Mwisho
Ndugu Wananchi;
            Mwisho, nawashukuru, kwa mara nyingine tena, Mheshimiwa Waziri Shamsi Nahodha na Meja Jenerali Muhuga kwa kunialika.  Nawashukuru wananchi na viongozi mbalimbali wa Serikali na wa vyama vya siasa kwa kuja kwa wingi kushiriki katika sherehe za siku ya leo.  Na, kwa namna ya pekee nawashukuru wananchi wote waliotembelea maonesho ya shughuli zinazofanywa na JKT.    Mmejionea wenyewe na kusikia faida za kuwepo kwa JKT.  Basi tuendelee kuliunga mkono Jeshi letu, lipate mafanikio makubwa zaidi miaka 50 ijayo.
Asanteni kwa kunisikiliza
Via/lukwangule blog

NANI KAMA LOWASSA? ACHANGISHA FEDHA AVUKA MALENGO MWANZA

PATA PICHA NA MAELEZO KAMILI


GUMZO LENYEWE
Picha hizo za Lowassa ambazo zimeenea mtandaoni, zimepokea maoni mbalimbali huku wengi wakiwa na maswali yaliyokosa majibu ya moja kwa moja.
Hata hivyo, asili ya picha hizo zilizombadilisha mwonekano Lowassa ni mtandao mmoja wa kijamii ambao umetupia picha na maelezo kwamba, mbunge huyo ambaye kasi yake ya kisiasa nchini haishikiki, alikuwa akipongezwa na Kiongozi wa Sunni al Jamaa Afrika Mashariki, Shariff Hussein al Badawi kwa kumvika joho na kilemba baada ya kufanikisha harambee kwa ajili ya Kituo cha Redio Ikra kinachomilikiwa na Baraza la Waislam Tanzania (Bakwata) Mkoa wa Mwanza. 

ENEO LA TUKIO
Ishu hiyo ilijiri usiku wa Ijumaa iliyopita katika Ukumbi wa Hoteli ya Gold Crest jijini Mwanza hivyo kuondoa utata kwamba, alivaa vazi hilo na kuzama nalo msikitini kitendo ambacho baadhi ya watu walisema si sahihi kama mheshimiwa huyo hajabadili imani yake. Lowassa ni wa imani ya KKKT.NA GLOBAL PUBLISHER

ACHANGISHA FEDHA, AVUKA MALENGO
Katika harambee hiyo, Lowassa aliyekuwa jijini humo sanjari na wafanyabiashara wengine wa karibu yake, alifan
ikisha wadau kuchangia shilingi milioni 590 hivyo kuvuka lengo la milioni 500. Kwa hiyo shilingi milioni tisini zilizidi.
Kufuatia hali hiyo, Risasi Mchanganyiko lilizungumza na baadhi ya viongozi wa Kiislam ili kuwasikia wanaliongeleaje tuko la Lowassa kuvaa vazi hilo.

SKU zilizopita kabla ya Mfungo wa Mwezi Mtukufu wa Ramadhani, picha za Mbunge wa Monduli kwa tiketi ya CCM, Edward Lowassa akiwa amevaa mavazi ya Kiislam ya joho na hagali zimezua gumzo kubwa kwenye jamii wengi wakitaka kujua kama Waziri Mkuu Mstaafu huyo amebadili imani au la !.

Akizngumza na gazeti hili juzi, Shehe Mkuu wa Tanzania, Mufti Shaaban Simba alisema kitendo anachofanya Lowassa cha kusaidia jamii ni cha kiungwana na kinakubalika kwa kuwa analisaidia taifa.

“Kusaidia jamii kunakubalika na kila mtu na tunataka watu kama Lowassa wawe wengi katika nchi yetu. Narudia tena kusaidia jamii si vibaya hata kidogo tuige mfano huo,” alisisitiza Mufti Simba.

SHEHE WA MKOA WA DAR ES SALAAM
Shehe wa Mkoa wa Dar es Salaam, Alhaji Mussa akizungumzia tukio hilo alisema ni jema  kwa kuwa alichochangia Lowassa kitasaidia jamii ya Watanzania.

“Mheshimiwa Lowassa amechangia redio na kama itatumika vizuri taifa zima la Tanzania litafaidika. Amefanya jambo zuri ambalo watu wengine wanapaswa kuliiga. Ieleweke hakuchangia ibada kachangia huduma za jamii,” alisema shehe huyo.

SHEHE WA MKOA WA MWANZA
Naye Shehe wa Mkoa wa Mwanza ambako tukio la Lowassa lilifanyika, Salum Hassan Fareji kwa upande wake alimpongeza kiongozi huyo kwa uamuzi wake wa kuchangia redio hiyo kwa kufanya harambee iliyozaa matunda. “Alichokifanya (Lowassa) ni faraja kubwa kwetu sisi kama viongozi wa Kiislam, tunamuomba aendelee kuhudumia jamii,” alisema.

KIONGOZI WA SUNNI
Kiongozi wa Sunni al Jamaa Afrika Mashariki, Shariff Hussein Al Badawi amesema kitendo alichokifanya Lowassa ni thawabu kubwa kwa Mwenyezi Mungu na amewataka watu wengine kuiga uungwana huo.

JAMII INASEMAJE?
Baadhi ya Watanzania waliozungumza na Risasi Mchanganyiko kwa nyakati tofauti walisema kwao kiongozi kuchangia jamii ni vyema tu, mbaya kama katika kuchangia huko atakuwa anapiga kampeni ya nafasi au cheo anachokifukuzia.

“Mimi sidhani kama kuna tatizo, kiongozi yeyote anatakiwa kuisaidia jamii, awe tajiri au wa kipato cha kawaida, tatizo litaibuka kama kiongozi huyo atatumia nafasi hiyo kufanya kampeni,” alisema Slim Abood, mkazi wa Kijitonyama Dar.
    
KUHUSU LOWASSA
Siku za hivi karibuni, Mheshimiwa Lowassa amekuwa akifanya harambee mbalimbali kuchangia jamii. Maeneo ambayo amekuwa akiyagusa zaidi ni nyumba za ibada na makundi ya akina mama, lakini hivi karibuni alikutana na Machinga wa Jiji la Mwanza ambao aliwaahidi kuwajaza ‘mafedha’ kwa ajili ya kujiinulia vipato vyao.

NI KUUSAKA URAIS ?.
Kufuatia hali hiyo, baadhi ya watu wakivitumia vyombo vya habari wamekuwa ‘wakitabiri’ kwamba, Lowassa anafanya harambee hizo kwa lengo la kuusaka urais wa Tanzania mwaka 2015.

Hata hivyo, Lowassa mwenyewe hajawahi kuweka wazi msimamo wa kugombea urais mwaka huo. 

LOWASSA AZUNGUMZA NA RISASI MCHANGANYIKO
Baada ya yote, Risasi Mchanganyiko lilipata nafasi ya kuzungumza na Mheshimiwa Lowassa kwa njia ya simu ya kiganjani na kumuuliza nini madhumuni yake ya kufanya harambee ya kuchangia redio hiyo ambapo alikuwa na haya ya kusema:
“Nimeamua kufanya harambee ile kwa sababu ni redio ya dini. Unajua unapochangia redio ya dini, yoyote ile maana yake itaweza kutoa vipindi bora vya kuelemisha jamii yote.
via/jumamtanda blog