Monday, May 27, 2013

BREAKING NEWS -----NANE WAFARIKI DUNIA KWA AJALI

Picture
Lory lililopata ajali na kusababisha vifo


Na Nathan Mtega,Songea

 WATU  nane wamefariki dunia kwa ajali ya gari iliyotokea Mei 27 mwaka huu majira ya saa 7 usiku katika kitongoji cha Bombambili kata ya Hanga wilayani Namtumbo mkoani Ruvuma.

  Kwa mujibu wa mashuhuda wa ajali hiyo walisema kuwa watu zaidi ya ishirini walikuwa wakisafiri kwenye gari la mizigo aina ya Isuzu lenye namba za usajili T 697 ABC lililokuwa likitoka wilayani Namtumbo kuelekea Songea likiwa limebeba magunia zaidi ya thelathini ya ufuta pamoja na abiria hao wakiwemo wamiliki wa mzigo huo.

  Walisema kuwa baada ya gari hilo kufika eneo hilo ghafla liliacha njia na kugonga karavati na kupinduka na baada ya kupinduka mzigo huo wa magunia ya ufuta uliwafunika watu hao na kusababisha vifo vya watu saba papo hapo huku mwingine mmoja akifariki baada ya kufikishwa hospitali ya rufaa ya mkoa wa Ruvuma.

Kamanda wa polisi wa mkoa wa Ruvuma Deusdedit Nsimeki akithibitisha kutokea kwa ajali hiyo alisema kuwa uchunguzi wa awali unaonyesha kuwa chanzo cha ajali hiyo ni mwendo kasi wa dereva wa gari hilo uliosaababisha ashindwe kuumudu usukani ingawa uchunguzi zaidi unaendelea kufanyika.

 Aidha aliwataja watu waliofariki dunia kuwa ni Bakali Bakali,Athman Awaja,Matola Gwaja,Jawadu Ntambo,Adamu Hamimu,Raika Abediul na wengine ni Musa Mdalali,na Abdalah Magongoni

 Naye Mganga Mkuu mfawidhi wa hospitali ya rufaa ya mkoa wa Ruvuma Dkt Benedict Ngaiza alithibitisha kupokea majeruhi kumi na moja wa ajali hiyo ambapo majeruhi wawili walitibiwa na kuruhusiwa huku majeruhi tisa akiwemo mtoto mwenye umri wa miaka 11 akiwa amevunjika miguu yote miwili wanaendelea kupatiwa matibabu hospitalini hapo.

Mwisho.

No comments:

Post a Comment