Wednesday, May 1, 2013

MWAMBUNGU AWASTUKIA WAWEKEZAJI


MATREKTA YAKIWA KAZINI KUCHIMBA MAKAA YA MAWE HUKO KIJIJI CHA MTUNDUWALO, KATA YA RWANDA WILAYA YA MBINGA- RUVUMA



Na Nathan Mtega,Mbinga.
MKUU wa Mkoa wa Ruvuma Said Mwambungu amelazimika kuufunga kwa muda mgodi wa makaa ya mawe wa kampuni ya TANCOAL  baada ya wananchi wa kijiji cha Mtunduwalo kata ya Ruanda Wilaya ya Mbinga kumtaka aufunge mgodi huo mpaka watapolipwa madai yao ya muda mrefu ya fidia pamoja na kuyaweka mazingira yao katika hali inayostahili kwa matumizi ya binadamu.
 
 Mwambungu alichukuwa uamuzi huo kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye viwanja vya shule ya msingi Mtunduwalo ambao ulihudhuriwa na mamia ya wanakijiji hicho wakiwemo viongozi wa kamati za ulinzi na usalama za Wilaya ya Mbinga  na Mkoa pamoja na viongozi wa vyama vya siasa.

Mapema Mkuu wa Wilaya ya Mbinga Senyi Ngaga akimkaribisha Mkuu wa Mkoa Mwambungu ili aweze kuongea na wananchi kuhusu mgogoro uliopo kati ya wananchi na mwekezaji wa mgodi huo ndipo  alipoanza kwa kusema wananchi wa Mtunduwalo hoyee!wananchi wakajibu hoiiii!mpaka kieleweke kadhalika kwa mkuu wa Mkoa ambapo aliwataka kuwa watulivu wakati anapotaka kuwaambia nini serikali yao imefanya katika kulimaliza tatizo hilo.

Pamoja na Mkuu wa Mkoa kujaribu kuwatuliza wanakijiji hao lakini bado hali iliendelea kuwa mbaya baada ya wananchi hao kumshinikiza mkuu huyo wa Mkoa waende nae mpaka kwenye eneo la mgodi akaufunge na kama haitawezekana basi wapo tayari kufa kwa kupigwa risasi kuliko kufa kwa njaa wakati haki zao zipo zinadhurumiwa na viongozi wa serikali huku baadhi yao wakiugua magonjwa mbalimbali kutoka kunywa maji yenye chembechembe ya sumu ya madini ya makaa yam awe yanayochimbwa eneo la kijiji hicho.

Akitoa kero mbele ya Mkuu wa Mkoa  Mwambungu  mwananchi Erick Mapunda alisema kuwa wamechoka na ahadi hewa za mwekezaji ambazo kila kukicha imekuwa ni siasa hivyo ujio wa Mkuu wa Mkoa huyo uwe ni hitimisho la kwenda kuufunga mgodi huo mpaka hapo watapotimiziwa ahadi walizoahidiwa pamoja na kuwalipa fidia wanazoidai kampuni ya TANCOAL.



Joseph Messa alieleza kuwa yeye kama mwananchi wa kijiji hicho ameshakata tama ya maisha kwa sababu hali ya kijiji chao ni mbaya kutokana na kukosekana kwa miundo mbinu ya barabara,maji,shule pamoja na zahanati kwani watoto wao wamekumbwa na magonjwa ya kichocho ambayo hawajui yanasababishwa na nini na kwamba wamekuwa wakinywa maji ya sumu tangu mgodi huo uanze kufanya kazi licha ya kuwa malalamiko hayo walishapewa viongozi wa serikali ya kijiji,Wilaya na Mkoa.



Kwa upande wake  Benedina Komba alisema kuwa tangu mgodi huo uanze kufanya kazi wananchi wa kitongoji cha Nkaya walipewa ahadi ya kuhama maeneo yao kwa muda kwa madai kuwa wataonyeshwa maeneo mengine ambayo wangepewa fidia ili wakajengee mahali pengine jambo ambalo mpaka sasa halijatekelezeka huku wakiangaika na watoto kutokana na njaa kwa kuwa eneo walilokuwa wakilima kuchukuliwa na kampuni hiyo.



 Wosteri Mapunda alielekeza shutuma nzito kwa waandishi wa habari wa Mkoa wa Ruvuma kwa kutoandika habari za mgogoro huo tofauti na waandishi wa Mkoa wa Arusha ambao wamekuwa wakiandika habari za mgogoro wa Loliondo ambapo serikali baada ya kusikia kwenye vyombo vya habari ilihamia Loliondo ili kumaliza tatizo lililopo na kwa nini Mtutunduwalo ishindikane kwa muda wa miaka mitatu sasa.



Aidha  Johoni Nyimbo alimnyooshea kidole Mbunge wa jimbo la mbinga mashariki  Gaudensi Kayombo na kumkumbusha ahadi aliyowaahidi wananchi wa kijiji hicho mei 19 mwaka 2011 kwenye mkutano wa hadhara kuwa endapo wanakijiji hao hawatalipwa fidia wanazodai atajiuzuru nafasi aliyonayo ya ubunge na kumtaka ajiuzulu nafasi ya ubunge mara moja jambo ambalo lilimpandisha hasira na  baada ya kauli iyo alilazimika kusimama ili kutoa ufafanuzi wa kauli yake hali ambayo isababisha kuwapandisha hasira wananchi hao na kuanza kumzomea.



Hata hivyo Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Ruvuma ambaye pia ni Mwenyekiti wa halmashauri ya Wilaya ya Mbinga  Oddo Mwisho naye alikumbwa na adha ya zomea zomea hiyo baada kusimama na kuanza kujieleza kuhusiana na jitihada za chama cha CCM na Serikali yake ya Wilaya na Mkoa kuwa kwa muda mrefu wamekuwa wakifanya mazungumzo kupitia Wizara ya nishati na madini,Shirika la maendeleo ya Taifa (NDC) pamoja na mwekezaji wa kampuni hiyo ya TANCOAL kwa lengo la kumaliza mgogoro uliopo kati ya mwekezaji na wananchi.



Kufuatia vurugu zilizojitokeza kwenye mkutano huo mkuu wa Mkoa  Mwambung alilazimika kusitisha mkutano huo kwa muda na kuwataka wananchi hao warudi eneo la mkutano baada ya nusu saa ili apate nafasi ya kujadiliana na kamati yake ya ulinzi na usalama na baadae baada ya nusu saa kupita mkutano ulianza ambapo Mkuu wa mkoa Mwambungu aliwaeleza wanakijiji hao kuwa amesikia maoni yao na amefikia hatua ya kuufunga mgodi huo kwa muda hadi hapo madai yao mbali mbali yatakapofanyiwa kazi na kutekelezwa.

Mwisho.

 

No comments:

Post a Comment