Wednesday, June 26, 2013

UJIO WA RAIS OBAMA TANZANIA, MAANDALIZI SIO MCHEZO

 
Rais wa Marekani, Barack Obama.
Na Mwandishi Wetu UJIO wa Rais wa Marekani, Barack Obama ni kufuru tupu, kiasi cha fedha ambacho kinachotumika kugharamia ziara yake peke yake kinazidi mara mbili ya kile kilichoteketea pale mtangulizi wake, George W. Bush, alipotembelea nchini mwaka 2008.
Obama, rais wa kwanza mwenye asili ya Bara la Afrika kutawala Marekani, atawasili nchini Julai Mosi, mwaka huu na kufanya ziara ya siku mbili.
Inaaminika kuwa Bush alipokuja nchini, msafara wake uliigharimu Marekani kiasi cha dola milioni 50 (shilingi bilioni 80) lakini Obama na timu yake watatumia mara mbili ya hapo, yaani dola milioni 100 (shilingi bilioni 160).
Hesabu hiyo, ilimtisha hata Mbunge wa Singida Mjini (CCM), Mohamed Dewji ‘Mo’ ambaye aliandika kwa mshangao katika akaunti yake ya Twitter, Jumamosi iliyopita: “Ujio wa Obama Tanzania utaigharimu Marekani dola milioni 100.”
UKUBWA WA MSAFARA
Kwa mujibu wa ziara mbalimbali ambazo Obama alishazifanya tangu alipoingia madarakani Januari 2009, msafara wake huwa na watu zaidi ya 800.

Obama ambaye ni Rais wa 44 wa Marekani, akiwa na mkewe, Michelle, huongozana na watu 500 ambao ni watumishi wa kawaida wa Ikulu ya Marekani, White House.
Katika wahudumu hao 500, wapo madaktari sita pamoja na wauguzi wengine zaidi ya 30, wapishi na kadhalika.
Msafara wa Obama, haukamiliki bila walinzi karibu 300 ambao jukumu lao huwa ni kumlinda rais huyo kwa ukaribu zaidi.
Kutokana na hesabu hiyo ni wazi kuwa Tanzania itakuwa na msukosuko wa aina yake pale Obama atakapowasili Uwanja wa Kimataifa wa Julius Nyerere.
Hata hivyo, kwa vile ndege ya Rais wa Marekani, Air Force One, haina uwezo wa kubeba idadi hiyo ya watu, wengi wao watawasili kwa mafungu wiki hii ili kufanya maandalizi ya ujio wake.
Ulinzi wa Obama.
MASHUSHUSHU KILA KONA
Kuelekea siku ya ujio wa Obama, Jiji la Dar es Salaam, limeshawekwa chini ya ulinzi, mashushushu kutoka Marekani wametanda kila kona kuhakikisha rais huyo hapatwi na zahama yoyote akiwa nchini.
Maofisa wa CIA (Central Intelligence Agency) ambao kiuhalisia ndiyo Idara ya Usalama wa Taifa la Marekani, wanadaiwa kuwepo nchini tangu Januari, mwaka huu, lengo likiwa ni kuratibu na kuhakiki usalama wa nchi.
Vilevile inadaiwa, makomandoo wapatao 400 kutoka Taasisi ya Upelelezi ya Marekani, FBI (Federal Bureau of Investigation), waliwasili nchini kwa mafungu kuanzia mwishoni mwa mwaka jana, jukumu lao likiwa ni kuweka mambo sawa.
Madai hayo yanajengwa na hoja kwamba hata pale FBI walipojitolea kutoa mchoro wa mtu aliyedaiwa kumpiga risasi na kumuua Padri Evarist Mushi, Machi mwaka huu, ilikuwa ni kwa haraka sana.
“Wale FBI walikuwa hapahapa Tanzania ndiyo maana walijitolea kutoa mchoro wa Padri Mushi kwa haraka sana, ingekuwa wapo Marekani wasigejitolea haraka vile.
“Sema sasa ilikuwa siri kubwa. Taarifa za ujio wa Obama kuja zipo tangu mwaka jana ila zilifanywa siri kwa sababu za kiusalama,” alisema ofisa mmoja wa Ikulu ya Tanzania kwa sharti la kutotajwa jina lake gazetini.
Gari la Obama.
ANAKUJA NA MAGARI 21
Kwa mujibu wa taarifa za ziara za Rais  Obama, kiongozi huyo husafiri na jumla ya magari 21.
Obama husafiri na gari lake binafsi kama Rais wa Marekani aina Limousine Cadillac, ambalo halilipuki wala kuharibika hata likipigwa na bomu.
Gari hilo likilipuliwa na bomu, matairi peke yake ndiyo huungua lakini hubaki na rimu ambazo hutembea kwa umbali wa kilometa 500 bila wasiwasi.
Limousine Cadillac ambalo ni toleo maalum la mwaka 2009 kwa ajili ya Obama pekee, huambatana na magari mengine 20.
Kutokana na tafsiri hiyo, Obama akiwa nchini, atakuwa na msafara wake uliokamilika na unaojitegemea kwa asilimia 100.
MAGARI 21 YATAKUJA VIPI?
Habari zinasema kuwa Limousine Cadillac ndilo litakalokuja na Air Force One, Julai Mosi, mwaka huu, mengine 20 yatawasili kabla ya ujio wa Obama.
Inaelezwa kuwa sababu ya magari hayo 20 kutokea Marekani ni kwamba utaratibu wa White House unaeleza kuwa msafara wa Rais wa Marekani ndani ya nchi unapaswa kufanana na wowote ule anapokuwa nje ya nchi.
Habari zinaeleza kuwa magari hayo 20, yatawasili na manowari kubwa ya Marekani ambayo inategemea kuwasili nchini wakati wowote kupitia Bahari ya Hindi.
Inaelezwa kuwa kazi nyingine ya manowari hiyo ni kudumisha usalama baharini, kuhakikisha watu wenye lengo la kufanya uvamizi hawafanikiwi kwa njia ya majini katika kipindi hiki cha siku chache kabla ya ujio wa Obama na hata pale akiwepo.
HOTELI ZA NYOTA TANO ZAJAA
Uchunguzi wa Risasi Mchanganyiko  umebaini kuwa ujio wa Obama umekuwa na neema kwa hoteli zenye hadhi ya nyota tano ambazo karibu zote zimekodiwa jumla.
Hoteli hizo zimechukuliwa na Marekani kwa ajili ya watu watakaombatana na Obama ikiwemo wahudumu pamoja na walinzi mbalimbali.
Inaelezwa, baadhi ya hoteli kuna wateja walihamishwa wiki mbili kabla ili kupisha wageni kutoka Marekani ambao wamekuwa wakiwasili nchini kwa mafungu.
WENYE MAGARI MAPYA WAULA
Uchunguzi zaidi umebaini kuwa wamiliki wa magari mapya yenye nafasi, hususan Toyota Noah, kwao ni neema ya aina yake.
Risasi Mchanganyiko limebaini kuwa wenye magari hayo hutakiwa kuripoti Ubalozi wa Marekani nchini kisha vyombo vyao hupimwa kuona uzima wake.
Habari zinasema, kila mwenye gari ambalo litafuzu vipimo, atalipwa shilingi 200,000 kwa siku katika kipindi chote litakapotumika katika ziara hiyo ya Obama.
BUSH NAYE ANAKUJA
Katika hatua nyingine, Bush ambaye ni Rais wa 43 wa Marekani, atawasili nchini hivi karibuni.
Hii ina maana kuwa kipindi ambacho Obama atakuwepo nchini, Bush naye atakuwepo ndani ya Tanzania.
Bush yeye anakuja kwa ajili ya kuhutubia mkutano wa wake za marais mbalimbali duniani ambapo imeelezwa kuwa mke wa Obama, Michelle, naye atahudhuria.
 KARIBU OBAMA
Ujio wa Obama ni fahari ya Tanzania kwamba nchi yetu ni salama na inavutia ndiyo maana hata kiongozi huyo wa taifa kubwa kabisa duniani, ameweza kushawishika kuja.
Karibu sana Tanzania Rais Obama. 
via/boss ngasa blog

No comments:

Post a Comment