Monday, April 29, 2013

WAZEE WASTAAFU WALIA NJAA RUVUMA



Baadhi ya Wazee wakielekea NMB Tawi la Matogoro, Songea wengine pale mbele kushoto karibu na Mashine za ATM nje wakiwa wamekaa chini wsijue la kufanya baada ya kukosa fedha zao za Pensheni. (Picha na Juma Nyumayo)










Mzee Mstaafu Bw. Holela maarufu kama Mkandamkanda (Kulia) akimsimulia kadhia ya kukosa Pensheni Mhariri waTujifunze  Kanda ya kusini, Bw. Christian Sikapundwa (Kushoto) yeye ni miongoni mwa wastaafu wanaolia  njaa Mkoani Ruvuma 

Baadhi ya Wazee wastaafu wakikatisha mtaa kuelekea Benki ya NMB Tawi la Matogoro, Songea upande wa kushoto leo kuangalia kama Pensheni yao imetoka. (Picha na Juma Nyumayo)






 
 









NA Juma Nyumayo, Songea.

KATIKA hali ya kutia simanzi na masikitiko makubwa, wazee wastaafu wa serikali mkoani Ruvuma, wanaendelea kulia njaa baada ya kukosa fedha zao za Pensheni wiki hii.

Wazee hao wanaotoka karibu kila kona za mkoa huu, wakisafiri umbali mrefu  kwa nauli za kukopa na hata wale wanaotembea kwa miguu wameambulia patupu.

Wakizungumza na mtandao huu, kwa nyakati tofauti karibu na Tawi la Benki ya NMB, Manispaa ya Songea leo,  wamesema hivi sasa wanakabiliwa na matatizo makubwa kwa wale waliowakopa na changamoto ya kujikimu hapa mjini na familia walizoziacha huko walikotoka.

" Hali yetu ngumu sana kifedha, kama ujuavyo sisi ni wazee hutegemea Pensheni kila baada ya miezi mitatu, huu ni karibu  mwezi wa nne, hakuna kitu," alilalamika Mzee Mstaafu ajulikanae kwa jina moja tu la Mapunda toka Wilaya mpya ya Nyasa.
Mzee mapunda anasema alikuja Songea toka Aprili 25 mwaka huu kufuata Pensheni yake akiwa na bajeti ya Nauli, Madeni kibao yenye riba toka huko Mbambabay - Nyasa.

Mzee Mwingine ni aliyekuwa mtumishi wa Idara ya Kilimo, Driver maarufu  Manispaa ya Songea, kwa Jina la Mkandamkanda, ambaye yeye amepaza sauti kuwa hivi sasa hajui mkewe amjibu nini maana hawana kitu na hategemei kukopeshwa.

"Sielewi mke wangu ni mjibu nini! maana hamna kitu," alilalamika Mzee mkandamkanda aliyestaafu kazi mwaka 2007.
Wazee hawa ambao walilijenga taifa hili kwa nguvu moja baadhi yao walikwenda kuulizia Hazina Ndogo Ruvuma kama serikali imetoa pesa yao. Wengi wao wameelezwa kuwa serikali imetoa pesa na kupelekwa NMB Tawi la Songea tayari kwa malipo.
" Tumejibiwa pesa zimepelekwa NMB, na NMB tukiangalia salio hamna pesa," alisema Mkandamkanda.

"hapa sisi tunapigwa danadana kama mpira, hali zetu ngumu na amini kila mzee ni mgonjwa kwa kukosa nguvu za kifedha na afya," alisema Mkandamkanda kwa hisia kubwa.
Tatizo la kucheleweshewa Pensheni wazee linawakosesha raha si wao tu bali hata waajiriwa waliopo kazini kwani ni wazee wastaafu watarajiwa.

Wazee hao kwa niaba ya wenzao wameliomba Bunge linaloendelea Dodoma na wizara husika kuhakikisha wanapewa Fedha zao mapema ili waweze kujikimu kimaisha.

Uchunguzi wa Blogu hii umeoneshwa wastaafu kukatishwa tama na hatua za polepole zinazochukuliwa kushughulikia fedha hizo za Pensheni na kuwafanya baadhi yao wajutie utumishi uliotukuka walipokuwa waajiriwa.
Mwisho

 


No comments:

Post a Comment