Tuesday, August 30, 2011

Gari lapinduka laua sita na kuwaunguza moto wawili wajeruhiwa



Sita wamekufa na kuteketea kwa moto baada ya gari lao kupinduka Mbinga
Na Juma Nyumayo, Songea

WATU sita wamefariki papo hapo na wengine wawili akiwemo mtoto wamejeruhiwa vibaya baada ya gari walilokuwa wakisafiria kupinduka na kuwaka moto katika kijiji cha Chunya kilichopo wilayani Mbinga mkoani Ruvuma.
Kamanda wa polisi mkoa wa Ruvuma Machael Kamuhanda (Pichani) amesema kuwa tukio hilo limetokea juzi (28.8.2011) majira ya saa 12 jioni.
Kamuhanda amebainisha miongoni mwa waliofariki miili yao kuwa imeuungua vibaya huku maiti hizo zikiwa hazitambuliki.
Kamuhanda alisema kuwa tukio hilo limehusisha Gari lenye namba za usajili T 270 BDG Landrover likiwa linaendeshwa na Dereva Stevin Ngoko (32) kupinduka na kuwaka moto na kusababisha vifo vya watu sita papo hapo katika kiji cha Chunya barabara iendayo Mbambabay toka Mbinga.
Kamanda Kamuhanda amewataja waliojeruhiwa katika ajari hiyo kuwa ni Jeremia Masalo (38) mkazi wa nchi jirani ya Msumbiji na Anna Godrfei (3) mkazi wa Mbambabay ambao wote wamelazwa katika Hospitali ya Serikali ya Wilaya ya Mbinga kwa matibabu.
Alisema kuwa watu waliokufa majina yao hayajaweza kufahamika kutokana na maiti hizo kutotambulika kwa kuwa zimeungua vibaya na zote zimepelekwa katika chumba cha kuhifadhia maiti katika hospitali ya wilaya hiyo.
Kamanda Kamuhanda alisema kuwa chanzo cha ajali hiyo ni mwendo kasi ambao ulimsababishia dereva wa gari hilo kushindwa kumudu usukani na kwamba jeshi lake linaendesha msako wa kumtafuta dereva wa gari hilo Bw. Ngoko ambaye alitoroka mara tu baada ya kutokea ajali hiyo.
MWISHO.

Monday, August 29, 2011

Maskini Diwani akamatwa akitetea ardhi ya wananchi



MASIKINI! POLISI WAMKAMATA DIWANI ANAYETETEA WANANCHI WASIPOKONYWE ARDHI MSHANGANO SONGEA

Na, Juma Nyumayo, Songea

JESHI la Polisi mkoani Ruvuma liliwakamata na kuwahoji zaidi ya masaa matatu wakazi wawili wa Kata ya Mshangano na Diwani wa kata hiyo Mheshimiwa Faustin Mhagama kupitia Chama cha Mapinduzi(CCM) (Pichani) kwa tuhuma za kutangaza maandamano ya amani ya wananchi wa kata hiyo wakidai kupimiwa ardhi yao na Kampuni ya Ardhi Plan na kumtaka Waziri mkuu Mizengo Pinda kuwatimua kazi Mkurugenzi wa Manispaa ya Songea na Afisa Mipango Miji wa Manispaa hiyo ambao wameonyesha dhahili kutaka kuwadhulumu maeneo yao.

Wakazi hao waliokamatwa na polisi ni Suzo Luoga ambaye alikuwa ni dereva wa gari ya matangazo lenye namba za usajili T 295 AJS aina ya Chesar mark II,Joseph Haule ambaye alikuwa mtangazaji na Faustine Mhagama ambaye ni Diwani wa kata hiyo ambao wote walikamatwa wakiwa kwenye gari hilo ambalo lilikuwa linapita kwenye mitaa ya kata hiyo kuwatangazia uwepo wa maandamano makubwa

Mmoja wa watuhumiwa hao Haule ambaye alikuwa mtangazaji alisema kuwa kazi hiyo alipewa na viongozi ambao wenyeviti wa serikali ya mitaa ya Namanyigu,Mshangano na Mitendewawa na kwamba shughuli hiyo ya utangazaji ilisimamiwa kikamilifu na Diwani wa kata lengo kuhakikisha ujumbe unawafikia wakazi wote wa kata hiyo

Naye wa Diwani wa Kata hiyo Mhe. Mhagama akizungumza na Mwandishi wa habari hii alikili kukamatwa na alidai kuwa yeye pamoja na wenzake walikamatwa na Polisi majira ya saa tatu usiku huko katika eneo la Bombambili Kadogoo wakitaka kuelekea Mshangano mara baada ya kumaliza matangazo yao na waliamriwa kuingia kwenye gari la Polisi wakiwa chini ya ulinzi mkali na kupelekwa kwenye kituo kikubwa cha Polisi

Alisema kuwa mara baada ya kufikishwa kituoni hapo waliamliwa kuvuliwa viatu,mkanda na kuanza kupekuliwa na kasha kuwekwa mahabusu ambapo baadae alifika Kaimu Mkuu wa Polisi wa Wilaya akiwa ameongozana na Askari Kanzu wawili ambao walianza kuwahoji hadi saa tano na nusu usiku ndipo walipoambiwa wawatafute watu wa kuwadhamini ambapo Mwenyekiti wa Kamati ya Mipango Miji wa Halmashauri ya Manispaa ya Songea James Makene pamoja na Diwani wa Viti maalum Rehema Milinga walifika kituoni hapo na kuwadhamini

Kwa upande wake Makene ambaye pia ni Diwani wa Kata ya Matarawe aliuambia mtandao huu kuwa kitendo cha kuwakamata Diwani na wenzake ni uonevu mkubwa na kinyume na utawala bora kwa kuwa Serikali ya Kata ya Mshangano ilipeleka barua ya kuomba kibali cha maandamano toka tarehe 19.8.2011 ambapo mpaka wanakamatwa walikuwa hawajapewa barua wala maelezo ya aina yoyote jambo ambalo liliashiria kukubaliwa

Naye Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Ruvuma Michael Kamuhanda alisema kuwa wananchi wa kata ya Mshangano waliomba kibali cha kutaka kufanya maandamano makubwa ya amani lakini katika barua yao ilionyesha mapungufu mengi ikiwa ni pamoja na kutoeleza tarehe,muda na njia ambayo maandamano yatapita

Kamuhada alisema kuwa tayari Serikali ya Kata ilipewa barua ya maelekezo na Jeshi la Polisi yenye kumbukumbu namba.SOA.3.6/65 ya tarehe 25.8.2011 ambayo ilipokelewa na Diwani wa kata hiyo majira ya saa mbili usiku
MWISHO


Wafanya maomba wasipokonywe ardhi!

Mhesshimiwa Diwani wa Kata ya Mshangano (wa pili toka kushoto) akishiriki maombi na wananchi wengine mara alipo achiwa na Polisi waliomkamata na kumshikilia kwa saa zaidi ya tatu kwa kile walichokiita uchochezi. Wengine ni wenyeviti wa Serikali za Mitaa wa Mitendewawa, Bw. Bernado, Mtaa wa Namanyigu Bw. Malindisa na Mtaa wa Mshangano Bw. Mangwe anayeendesha maombi hayo kwa kuinua mkono juu ili Mungu awasaidie Uongozi wa Mkurugenzi wa Manispaa Nachoa Zakaria na Ofisa Mipango Miji wake Castory Msigala amabao ni kikwazo cha mpango wao wa kurasmishiwa makazi yao wafukuzwe kazi na Waziri Mkuu, Mheshimiwa Mizengo Kayanza Peter Pinda.


Thursday, August 25, 2011

Maandamano Makubwa yaja kumg'oa Mkurugenzi Manispaa Songea






Mwenyekiti Paul Mangwe akisoma tamko mbele ya waandishi hawapo pichani. kushoto kwake Mwenyekiti wa Serikali Mitendewawa B)





Maandamano kumg'oa Mkurugenzi Manispaa


















Na Juma Nyumayo,Mshangano- Songea







WANANCHI wa Kata ya Mshangano, Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma wanatarajia kufanya maandamano makubwa ya amani ya kumtaka Waziri Mkuu Mizengo Pinda kumshinikiza Mkurugenzi wa Manispaa ya songea atoe kibali ca kupimiwa ardhi yao na kuwang’oa kazi huyo Nachoa Zakaria na , Afisa Mipango Miji wake Castory Msigala kwajili yakuwa kikwazo cha maendeleo ya wananchi.

Akisoma tamko la wenyeviti wa serikaili za mitaa wa kata ya Mshangano ambayo imekumbwa na mgogoro mzito wa ardhi, Mwenyekiti wa serikali ya Mtaa wa Mshangano, Paul Mangwe alisema kuwa (kesho) leo wanataria kuandamana kwa amani kuanzia ofisi ya kata hiyo hadi kwa Ofisi ya Mkuu wa wilaya ya Songea Thomas ole Sabaya, kumfikishia ujumbe wa kutaka kupewa kibali cha kupimiwa ardhi yao na kumuomba Waziri Mkuu kuwang’oa viongozi hao wawili ambao wamekuwa kikwazo kwa zoezi hilo.

“ Sisi wenyeviti wa serikali za mitaa ya Mitendewawa, Namanyigu na Mshangano tulishaomba kibali kwa OCD wa Songea kumjulisha kuhusu maandamano ya amani, kibali tutapata na hata kama hakitapatikana wananchi wamedai lazima waandamane kesho(Leo),” alisema Mangwe mbele ya waandishi wa habari ofisini kwake.

Alisema ifahamike kuwa wananchi wa kata ya mshangano tangu walipo kutana Agosti 13 mwaka huu walimtaka Mkurugenzi huyo awe amesaini michoro na kibali cha kuiruhusu Kampuni ya Ardhi Plan ltd yenye Makao makuu Dar es Salaam ambayo imekwisha wahi kufanya kazi kama hiyo kwenye Kata ya Mwenge Mshindo mjini hapa iweze kuwapimia wananchi maeneo yao ambayo wamesitisha shughuli ya kuyaendeleza tangu Disemba 2010.

Katika taarifa hiyo Wenyeviti wa Mitaa wa Kata hiyo walisema kwakuwa Mkurugenzi Nachoa na Afisa Mipango Miji wake Msigala wamekaidi matakwa ya wananchi wenye ardhi wa kata ya Mshangano kushindwa kujibu barua ambazo walizipeleka za kutaka kupimiwa ardhi takribani miezi tisa sasa wameshindwa kumuelewa ni kitu gain anachotaka kutoka kwa wakazi wa kata hiyo.

“Tunapata mashaka makubwa na kukosa imani na Viongozi hao wawili(Nachoa na Msigala) kwani pamoja na kutokujibu barua zetu lakini mazingira yamejionyesha kuwa wao wana maslahi binafsi,” walisema wenyeviti hao katika mkutano na waandishi wa habari.

Hata hivyo, walisema wao wapo tayari kufa kuliko kuiachia ardhi ya wapiga kura wao waliowachagua mwaka 2009 katika uchaguzi wa serikali za mitaa kuwaletea maendeleo.

Walisema kuwa hawaoni mtu mwingine atakaye suluhisha mgogoro huu mkubwa uliodumu kipindi kirefu zaidi ya mtoto wa mkulima Waziri Mkuu Mizengo Pinda mwenye uchungu na watu wanyonge hapa nchini.

Walisema wameshangazwa sana na viongozi wa serikali ya mkoa wa Ruvuma kulifumbia macho swala zito kama hili na hivi sasa wameona wana mtu mmoja tu ambaye wanaamini ana ujasiri wa kumfikishia ujumbe waziri Mkuu na si mwingine bali ni DC wa Songea Thomas Ole Sabaya ambaye hata kama atasema hana mafuta ya kwenda na kurudi Dodoma wao wako tayari kuchanga nauli hiyo ilimradi Waziri Mkuu Pinda apate ujumbe huo wa kutaka kurasmishiwa makazi yao badala ya kujenga kiholela kwenye eneo la Manispaa.

Kwa upande wake Kamanda wa Polisi Mkoa wa Ruvuma, Michael Kamuhanda, alisema kibali cha maandamano hayo hakijakamilika kwakuwa hakijakidhi matakwa kama yale ya kuonyesha njia, muda na tarehe ya maandamano.

Kamuhanda amefafanua kuwa tatizo hilo ni kubwa na tayari linatarajiwa kupelekwa kwenye kamati ya ulinzi na Usalama ya mkoa ili kuangalia wapi chanzo cha kuendeleza mgogoro huo hadi watu wafikie hatua ya kutaka kuandamana.
Mwisho

Wednesday, August 24, 2011

Fort Jesus (Ngome ya Yesu Mombasa! maajabu ya East Africa

Fort Jesus-Ngome ya Yesu pale Mombasa nchini Kenya ni miongoni mwa maajabu ya Afrika Mashariki.
Nilitembelea hapo na kama unionavyo nikiwa na Kibajaji hapo mitaani Mombasa nilikuwa katika harakati wa kutafuta na kuangalia maajabu na Urithi wetu wa hapa Afrika Mashariki.


Hilo Jengo ndiyo Ngome ya Yesu. Lilikuwa limepitia historia ndefu hadi kuwa gereza na Baadaye kubadilishwa kuwa eneo la Makumbusho linalovutia sana. hapo Mbele ni Bahari ya Hindi.








Nikishuka toka Taxi niliyokodi kunitembeza huko Old Mombasa, hapa kwetuTaxi hiyo huitwa Bajaji tu.







Thursday, August 11, 2011

Uzuri wa Jiji la Mwanza, Makoroboi Bwana!

Hapo nikiwa nasoma Gazeti la Mwanahalisi Makala iliyoandikwa na Mwalimu wetu wa Kufikiri, Bw. Ndimara Tegambwage kuhusu Mtaa huo wa Makoroboi na umbilikimo wa watawala. Makla hiyo inaeleza kuwa mtaa huo unataka kuuzwa na kuharibiwa sura yake kabisa, wachuuzi na wanunuzi hawatafaidi utamu uliowaasisi kuwepo hapo. Naomba uangalie picha hizo zinavyojieleza ni kama Mtaa wa congo pale Dar, lakini Makoroboi ni zaidi kuna vivuli vya miti na Mawe makubwa yanayoupamba mchochoro huo unaowatengenezea fedha sio machinga tu bali jiji lenyewe la Mwanza.
(Picha Zote na maelezo ya Juma Nyumayo)












Tuesday, August 9, 2011

Nilipokuwa Sengerema FM

Asanteni sana Sengerema FM, UNESCO, UNWOMEN n washiriki wote bila Kuwasahau Al Amin Yusuf, Rose Haji na wadau wote.




















Tukiwa angani, waandishi kama kazi!

Tukiwa angani Bw. Hassan Hashim (mwenye kofia) na Juma Nyumayo ama kweli Bw. Ali Haji Hamad Mjumbe wa Bodi ya UTPC ambaye kwa sasa anasoma Masters SAUT aliamua kupiga picha hiyo kwa kumbu kumbu yetu naomba niwashirikishe pia tuliyoyaona kabla hatujafuturu.

Mawingu mazito tukayachana, lakini Bw. Hassan Hashim akapiga picha kwaajili ya kuweka kwenye background ya Computer yake.



Hapa ilikuwa saa moja kasoro dakika 10 hivi, Bw. Ali Haji Hamad akatania kuwa jua lisingelizama na hatuwezi kufuturu bila kuzama kwa jua, ndipo Mary Edward akakumbuka wanafunzi wenzake wakati yupo Ujerumani, Ramadhani yao ilikuwa kasheshe kwani walifunga zaidi ya saa 14 jua halikuzama. Ni kipindi kile cha mchana mrefu ndipo waliamua kupiga simu kuuliza kwa wazazi wao huko Kenya kulikoni? Ama kweli walipata jibu kuwa wakati huo Kenya walikuwa wakisubiri kula Daku. Hata hivyo tulivyotua Uwanjani giza lilishaingia. Asante Mungu kwa kuwapa maarifa binadamu kuutawala ulimwengu.






Mwanza nako tatizo mafuta!

Hapa katika Picha nikiwa na waheshimiwa wajumbe wa Bodi ya UTPC, Bw. Hassan Hashim toka Tanga, Lucy Ogutu (kulia) toka Dar es Salaam na Mary Edward katikati akitokea Dodoma hivi sasa anafanyia kituo kikubwa kabisa cha Televiheni-ITV Dar Es Salaam wakijadili jambo jana Julius Nyerere International Airport kabla ya kwenda Mwanza.

Bw Juma Nyumayo akieleza jambo kwa Bw. Hassan Hashim aliyepiga pica hii.



Picha ya tatu Toka kulia Mary Edward, Hassan Hashim, Lucy Ogutu na Mimi Juma Nyumayo tukiwa uwanja wa Ndege wa kimataifa Dar es Salaam kabla ya kuruka kwenda Mwanza. (Picha na Ali Haji Hamad-Pemba)





Nimewasili Jiji la Mwanza, hakika linapendeza. Tatizo ni lilelile la mafuta. Petroli na Disel. Madereva wa Taxi hapa wanadai vituo vingi havina mafuta na kusababisha msururu wa magari kwenye vituo visivyo na mshipa wa kuwafuata hao wakubwa wao. Naunga mkono asilimia 100% Hoja ya Dharura kujadiliwa Bungeni kuhusu mafuta iliyotolewa na Mbunge Kijana ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati Nishati na Madini Mhe. January Makamba ambaye bila woga ameitka serikali kuonyesha uwepo wake. Hata hivyo wabunge wengi waliochangia nimewapenda kwa kile walichokionesha maslahi ya taifa bila kujali vyama walivyotoka. wbunge hawa ni pamoja na Mbunge wangu Mhe. Jenister Muhagama Mbunge wa Jimbo la Peramiho ambaye licha ya kuwa Katibu wa wabunge wa CCM alikuwa mkali akimaanisha Ibara ya 8 ya katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuwa serikali hupewa madaraka na wananchi hivyo wananchi lazima waione serikali yao inawajali katika kipindi kama hiki.

Asanteni sana Bunge huu ndio mwendo.

Juma Nyumayo