Sunday, June 6, 2010

Furaha David aukwaa Miss Ruvuma 2010

Juma Nyumayo, Makumbusho ya Taifa Majimaji Songea

Mlimbwende Furaha David (20) mwenye elimu ya Kidato cha nne ameibuka mshindi wa kwanza wa mashindano ya warembo ya Miss Ruvuma 2010.
Mlimbwende huyo licha ya kuvalishwa taji lake na aliyekuwa Miss Ruvuma mwaka jana, Glory Nicholous, alipewa zawadi ya kitita cha shilingi laki nne taslimu na ajira katika shirika la Ores- Tanzania linalohudumia watoto yatima na wanaoishi katika mazingira magumu.
Tukio hilo la kihistoria kwa warembo hao lilitokea usiku wa manane kuamkia Jumapili Juni 6, 2010 ambapo mgeni rasmi alikuwa Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Dkt Christine Ishengoma akiwakilishwa na Kaimu Katibu Tawala Mkoa wa Ruvuma Dkt. Anselm Tarimo.
Awali, Maelfu wa wakazi wa Manispaa ya Songea waliojitokeza kwenda kushuhudia mpambano huo katika viwanja vya wazi vya Makumbusho ya Taifa ya Majimaji eneo la Mahenge walipewa maelekezo na Mkurugenzi wa COTN Promotion & Entertainment, Miss Emmy Mssanja kuwa kulikuwa na washiriki 11 wenye vipaji na mategemeo tofauti ambao wataleta ushindani mkubwa ikilinganishwa na mwaka 2009.
Majaji watatu kutoka Dar es Salaam, wakiongozwa na Neema Kileo waliwasaidia watu kumpata mshindi huyo katika mpambano uliokuwa mgumu kutabiri kwani walimbwende hao waliokuwa na vipaji mbalimbali na urefu unaokimbiliana waliwaacha wakazi wa mjini hapa na vitongoji vyake kushindwa kumpata mshindi kabla ya saa 9.15 usiku.
Licha ya kupatikana kwa mlimbende huyo atakayepeperusha bendera ya ruvuma katika mashindano ya kanda na baadaye taifa, majaji hao waliridhika na Lilian Mbise (20) kuwa mshindi wa pili nakujinyakulia zawadi ya fedha taslimu shilingi laki tatu, na watatu aakawa mlimbwende Najat Makangila ambaye alijinyakulia donge la Shilingi laki mbili na ajira katika Shirika la COTN.
Mshindi wa nne na watano walipewa zawadi ya shilingi laki moja na nusu na wengine kifuta jasho cha shilingi laki moja kibindoni ikiwa ni zaidi ya ile ya mwaka jana ya shilingi elfu ishirini tu kwa kila mmoja.

No comments:

Post a Comment