Monday, December 16, 2013

WAPINGA MAENDELEO YA ELIMU MBINGA KUKIONA


Mkuu wa wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, Senyi Ngaga akitoa msisitizo wake mbele ya Wadau wa elimu wa wilaya hiyo(Hawapo pichani) katika ukumbi wa Umati uliopo mjini hapa, juu ya Katibu wa CWT wilaya humo kuwa ni kikwazo cha maendeleo ya elimu. 


Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

MKUU wa wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, Senyi Ngaga amemshukia Katibu wa Chama cha Walimu Tanzania (CWT) tawi la Mbinga Samwel Mhaiki, akidai kwamba ni kikwazo cha maendeleo ya elimu wilayani humo, kutokana na katibu huyo kupenda kuendesha migogoro na kuchonganisha walimu mashuleni.

Ngaga alisema hayo alipokuwa akizungumza na Wadau wa elimu, Kata ya Mbinga mjini juu ya kukuza maendeleo ya sekta ya elimu wilayani humo, katika hafla fupi iliyofanyika ukumbi wa Umati uliopo mjini hapa.

Alisema kuwa katibu huyo amekuwa kinara namba moja wa kupita mashuleni na kushinikiza walimu waache kufundisha (Wagome) hadi watakapolipwa madai yao, jambo ambalo alilieleza kuwa limekuwa likileta mgogoro usio na tija katika jamii.

Alieleza kwamba licha ya Mhaiki kuitwa mara nyingi ofisini kwake na kumtaka aache kuendeleza migogoro hiyo, anashangaa kumuona bado akiifanya.


“Tumemuonya mara nyingi huyo Mhaiki, lakini amekuwa bado akitusumbua kwa kuandika mabarua na kusambaza mashuleni akishinikiza walimu wagome waache kufundisha….tulimwambia serikali inashughulikia madai ya hawa walimu na watalipwa malumbano haya anayoyaendeleza sasa ningelikuwa na uwezo mimi kama Mkuu wa wilaya hii ningemhamisha, kwa sababu ni kikwazo kwa maendeleo ya elimu hapa wilayani, leo walimu wakigoma watoto wetu watafundishwa na nani”, alisema Ngaga.

Mkuu huyo wa wilaya awali alisema wilaya hiyo hivi sasa imejipanga katika kukuza kiwango cha elimu kwa shule za msingi na sekondari, ambapo kwa kushirikiana na ofisa elimu wa wilaya hiyo Mathias Mkali wamekuwa wakiendelea na mfumo wa watoto kujisomea wakati wa likizo (Makambi) kwa kila kata wilayani humo, hususani kwa watoto wa darasa la sita ambao wanaingia darasa la saba mwakani.

Alisema wazazi wameitikia wito kwa kiasi kikubwa juu ya suala hilo na kukubaliana kutoa michango ya chakula, katika vituo hivyo ambavyo watoto wao wanasoma wakati huu wa likizo.

Alisisitiza kuwa mtu yeyote atakayeonekana anakwamisha mikakati waliyojiwekea ya kukuza kiwango cha elimu wilayani Mbinga, yupo tayari kumwajibisha ili iwe fundisho kwa wengine wenye tabia kama hiyo

Friday, November 8, 2013

USTAWI WA KIJAMII NA UCHUMI RUVUMA

Kanisa la RC lililopo Sinai  Manispaa ya Songea, Kanisa hili lipo kando ya barabara iliyojengwa kwa kiwango cha lami toka pacha ya Peramiho kuelekea mjini Mbinga. Eneo hilo sasa limepanda thamani kutokana na usafiri wa uhakika jambo linalovutia wengi kwenda kuwekeza katika kilimo, ujenzi wa nyumba na ufugaji.

Hapa ndiyo "Dar Pori" Wilaya mpya ya Nyasa ni kilomita nane hivi kuingia Msumbiji. Kijiji hiki kimeibuka wakati wa machimbo ya Madini hasa dhahabu. hiyo barabara unayoione imechimbwa kwa majembe ya mkono. hakuna kinachoshindikana kwa binadamu wakidhamiria. Vijana wa bodaboda maarufu kama yeboyebo mkoani Ruvuma wakisubiri abiria "waliobongoa" waliopata fedha au madini  kuwapeleka Mbinga, Nauli yake ni Shs 40,000/- kwa abiria mmoja. Kazi kwelikweli. 

Mkazi wa Dar es Slaam, Bw. Jacob Silvesta Nyumayo, akionyesha mkungu wa ndizi huko kijiji cha Mgazini Kata ya Kilagano Songea Vijijini ambao umezaa vya kutosha licha ya kutotunzwa vizuri. Bw. Jacob anasema udongo wa Songea unafaa sana kwa kuzalisha ndizi za aina zote na huenda ndizi zingeliweza pia kuchangia pato la wananchi wa mkoa wa Ruvuma wakithubutu hasa wakati huu ambao sasa barabara zimefunguka na kuacha kutegemea zao moja tu la chakula kama mahindi na kutupilia mbali mihogo, mtama na mazao mengine. 

UKATILI , UNYAMA WA WANAUME


Mkurugenzi wa Kituo cha Msaada wa Sheria Songea,(Sopce) Fatuma Misango (mwenye kilemba cheusi) akimsikiliza mwanamke aliyejeruhiwa na mmewe bada ya kulewa huko ofisi ya mtendaji kata ya Tanga hivi karibuni.
HADITHI: Ulevi wa mume wake huyo ulimfanya achukue hatu ya kumpiga mwanamke huyo hadi kuzirai (Kuzimia) alivyomaliza kazi hiyo naye akalala fofo na kukoroma kama vile hakuna tukio alilolifanya hadi alipokuja kamatwa na mgambo kwa amri ya Afisa mtendaji wa kata hiyo.
KISA: Mwanaume huyo ana mtindo wa kwenda kulewa na kumuamuru mkewe asifunge mlango na komeo ili asipate tabu arejeapo nyumbani akiwa mitungi.
Hivyo mara kwa mara anaporudi husukuma mlango na kuingia ndani hujitupa kitandani akishapiga misosi yake hasa kama kuna kitoweo cha nyama.
SIKU YA TUKIO: Mwanaume huyo alikwenda kuzinyaka. kama ujuavyo pome si chai, usiku wa manane akarejea kwake. bahati mbaya akaukuta mlango u wazi haujaegeshwa. akaanza kulipuka kwa hasira kuwa ni vipi mlango ubaki wazi?
Mkewe akamjibu aliuegesha kama anavyofanya siku zote. Mume akasema haiwezekani ubaki wazi.
Mkewe akasema hapana mume wangu huenda upepo umeufungua.
Mume: Nasema haiwezekani, hapa atakuwa mwanaume amekimbia katoka humu ndani sikubali.
Kichapo kikaaanza kutembezwa.

Tuesday, November 5, 2013

IMANI BILA MATENDO? WANANCHI WA NYASA WALA KIAPO KUILINDA TANZANIA

Kutumikia wapiga kura: Mhe. Mkuu wa Mkoa wa Rukwa ambaye ni Mbunge wa Viti Maalum CCM Mkoa wa Ruvuma, Mhandisi Stella Manyanya akisalimiana na Mkurugenzi wa Blogu hii Jimboni Mjini Mbinga hivi karibuni wakati wa Ziara ya Mwenyekiti wa UWT  taifa ambaye pia ni Waziri wa Maendeleo ya jamii, Jinsia na watoto, Mhe. Sofia Simba
Angalia bango katika ukuta wa jengo linalosema "Imani bila Matendo, imekufa," Watanzania tunahitaji matendo zaidi.

Maeneo Magumu: Mhe. Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto, Sofia Simba akiwasili kijiji cha Dar Pori kwa wachimbaji wa madini wilaya mpya ya Nyasa. Waziri Sofia Simba amekuwa waziri wa kwanza mwanamke kuwasili eneo hilo gumu kufikika ambalo lipo mpakani mwa Tanzania na Msumbiji tangu nchi hii ipate huru 1961 (Kushoto) ni Mkuu wa Wilaya ya Nyasa Bw. Ernest Kahindi akimuongoza waziri huyo jukwaani wakati wananchi wakishangilia wakati wa ziara yake mkoani Ruvuma hivi karibuni.

Mikono Juu: Ni kiapo cha wananchi kuwa na  Utii wa kuipenda, kuitumikia na kuilinda Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kiapo hiki kilitolewa mbele ya waziri Simba huko Dar Pori wilaya ya Nyasa. Jengo la bati linaloonekana kwa mbali nyuma pale mlimani ni zahanati iliyojengwa kwa nguvu za wanakijiji hao wachimbaji wa madini.

MITIHANI YA KIDATO CHA NNE 2013

Tunawatakia heri ya mitihani ya kidato cha nne, 2013.
Huo ndio mwanzo wa kupanda mlima wa elimu ya juu.
kila la heri wote wanaofanya mitihani, wasimamizi, wazazi, na wadau wote.

Tuesday, September 10, 2013

WAANDISHI NA VINGOZI WA SERIKALI

Baadhi ya Waandishi wa habari wanaume wa mkoa wa Ruvuma, wakiwa katika picha ya pamoja na viongozi wa serikali ya Mkoa wa Ruvuma. (Mwenye shati la maua katikati) ni  Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma Said Thabith Mwambungu ( jirani yake kushoto )  ni Mkuu wa Wilaya ya Songea,  Bw. Joseph Joseph Mkirikiti . ( Picha kwa hisani ya Ruvuma Press Club)

MTIHANI WA DARASA LA VII - 2013

Tunawatakia wanafunzi wote wa Darasa la Saba (VII) nchini mtihani mwema wa kumaliza elimu ya Msingi. utakaoanza kesho Jumatano 11, September 2013.
Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dkt. Shukuru Kawambwa
Mtihani huu utakaofanyika kesho ndio msingi imara utakao amua kuendelea na masomo ya sekondari kwa mwanafunzi muhusika au la.
Miaka hii ya karibuni, tumeshuhudia waziwazi vyombo vyetu vya usalama vimewakamata baadhi ya wanafunzi, walimu na mara nyingine hata wazazi kushiriki kikamilifu katika uhalifu wa kielimu wa kuiba mitihani .
Uhalifu huu unafanywa ili kuwafaulisha wanafunzi wasiostahili na ndio wanaokuwa mizigo katika elimu yao ya upili. Jambo hilo ni baya kupita maelezo kwani elimu ni sawa na moto. Moto haukopeshi, ukiweka mkono katika kaa la moto utaungua mara moja. Na elimu hali kadhalika kama kijana hana uwezo akapitishwa kwa hila kuendelea na masomo, huwa ni mzigo kwa kijana huyo, familia yake pia taifa.
Tusishangae kuona madaktari feki, wahandisi kanjanja, walimu mizigo wanasiasa bomu na wengine kibao bila kusahau wakulima wasiozingatia kanuni za kilimo bora.
Lengo kuu hapa ni kuwatakia mtihani mwema, usio na hila za kuvujishwa wala kuvujisha.
Jamii ya wanaRuvuma inasema hakuna linaloshindikana, utavuna ulichopanda.
Mtihani Mwema 2013