Wednesday, August 22, 2012

Adhabu ya kifo siyo adhabu, ni uhalifu mwingine, Soma hii

Naona kuna mkondo wa kuua.



Sasa tuachane na wanaharakati na watetezi wa haki za binadamu. Tujaribu kufikiri bila vivuli vyao.



Twende kwenye hoja ya kuua:ANAYEUA ANASTAHILI KUUAWA.



Hicho ndicho kilio cha wachangiaji wengi. Kapoku kamuua Sadoko.



Sasa wanataka Kapoku auawe. Wanataka mahakama iamue kuwa Kapoku auawe mpaka afe. Mahakama inaamua hivyo. Serikali inayosimamia utekelezaji inatoa panga, msumeno, kamba au umeme na kuua Kapoku.


Nani sasa ameua Kapoku? Kwa ufupi mchinjaji ni serikali/utawala.
Twende mbele. Hoja ya wachangiaji wengi ni kwamba ANAYEUA AUAWE. Hivyo serikali iuawe. Kuua ni kuua - awe ameua masikini au tajiri, mtu binafsi au serikali. Ni uharamia tu.
Tutafute adhabu kwa aliyeua.


KIFO SIYO ADHABU. Kifo ni kuondosha maisha ya yule ambaye angefanya adhabu.


Tena angefanya adhabu angejutia alichofanya, angejifunza na jamii ingejifunza.


Aliyekufa hajifunzi. Hajutii kosa lake.


Kama Kapoku ameondoa maisha ya Sadoko na serikali imeondoa maisha ya Kapoku; hakika wote ni WAUAJI. Si vema kuishi katika dunia ya wauaji.
ndi.



(Nimeichukua hii toka http://www.ndimara.blogspot.com/ nasikitika sikuomba idhini toka kwake nimekosa kwa hili Juma Nyumayo)

Tuesday, August 21, 2012

KUFUNGIWA KWA GAZETI LA MWANAHALISI


Watetezi wa haki za binadamu, asasi za kijamii na wadau wakuu wa habari nchini, leo wameipa serikali siku saba kufungulia gazeti la MwanaHALISI, vinginevyo wataitisha maandamano ya kupinga hatua ya serikali kufungia gazeti hilo kwa muda usiojulikana, kuminya uhuru wa habari, haki za binadamu na utesaji wa wanaharakati.
Asasi ambazo zimetoa tamko la kutaka serikali ifungulie MwanaHALISI ni MISA, Legal and Human Rights Centre, Tanzania Human Rights Defenders Coalition, Human Rights National Association of Educators For World Peace and Citizen Rights Watch.
Tamko la asasi hizo ni kama ifuatavyo hapa chini:
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI 22 Agosti 2012
YAH: KUFUNGIWA KWA GAZETI LA MWANAHALISI

KWA mara nyingine tena, tumewaiteni hapa kuwaomba mtufikishie ujumbe wetu huu kwa watawala. Ujumbe wenyewe unahusu kufungiwa kwa gazeti la kila wiki la MwanaHALISI na kauli ya Waziri Mkuu Mizengo Kayanza Peter Pinda aliyoitoa bungeni, Alhamisi tarehe 16 Agosti 2012. Kama mnakumbuka vema, wakati akijibu swali bungeni siku hiyo, Waziri Mkuu Pinda alisema, “Serikali imechukua wajibu wake kulifungia gazeti hilo, na kwamba kama wahusika hawakuridhika na hatua iliyochukuliwa na serikali wana haki ya kukata rufaa kwa mamlaka za juu.”

Awali ya yote, tuseme wazi, kuwa hatukuridhika na majibu ya Waziri Mkuu kuhusu kufungiwa kwa MwanaHALISI. Majibu ya Waziri mkuu Pinda yamelenga kuahirisha tatizo, siyo kutatua. Kwanza, Waziri Mkuu anatetea uamuzi huo uliofanywa na sheria katili na kandamizi ya magazeti. Sheria inayonyang’anya uhuru wa kufikiri, uhuru wa kutoa maoni na uhuru wa kuwasiliana. Pili, Mheshimiwa Pinda anatumia sheria hiyo kutaka kuliangamiza gazeti hili ambalo limesifiwa kwenye ripoti mbalimbali za ndani na nje ya nchi ikiwamo ile iliyotolewa majuzi na Baraza la Habari Tanzania (MCT) inayochambua Mwenendo wa vyombo vya Habari nchini kwa mwaka 2011 inayosema katika ukurasa wa tisa:

“Pamoja na kusakamwa na serikali, MwanaHALISI limesimamia uandishi wake wa kuikosoa serikali.”

Serikali imelituhumu gazeti hili kwa kuchapisha habari ambazo inasema “zinakiuka” vifungu 32(1) (a), (c) – (d); 32(1)(c) na 36(1) vya Sheria ya Magazeti Na. 3 ya 1976. Habari hiyo inahusu kutekwa, kuteswa kinyama na hatimaye kutupwa katika msitu wa Mabwepande kwa kiongozi wa madaktari nchini, Dk. Steven Ulimboka. Hii ndiyo habari ambayo serikali inaita ya “uchochezi.” Yaani badala ya serikali inayojigamba ina mkono mrefu wa kumfikia yeyote kuutumia mkono huo kutafuta watuhumiwa waliotajwa na gazeti kuwa walifanikisha kutekwa kwa Dk. Ulimboka, imeamua kutumia mabavu kulifungia MwanaHALISI huku wakiacha maisha ya Dk. Ulimboka na wanaharakati wengine njia panda.

Serikali imechukua hatua hiyo, huku wakijua kuwa Ibara ya 18 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, 1977 kama ilivyorekebishwa na Sheria ya Mabadiliko ya 14 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (2005), ilipanua haki ya kutoa, kutafuta, kupokea, na kusambaza habari. Mabadiliko hayo yaliondoa kivizo cha “kwa mujibu wa sheria” Kila mtu- anao uhuru wa kuwa na maoni na kueleza fikra zake; anayo haki ya kutafuta, kupokea na kutoa habari bila ya kujali mipaka ya nchi; anao uhuru wa kufanya mawasiliano na haki ya kutoingiliwa katika mawasiliano yake.

Aidha, mabadiliko hayo yanatoa haki kwa kila raia ya kupewa taarifa wakati wote kuhusu matukio muhimu mbalimbali kwa maisha na shughuli za wananchi na pia kuhusu masuala muhimu kwa jamii. Hivyo basi haki na uhuru wa kujieleza, kupokea na kutoa habari haina vipingamizi ambavyo serikali inadai kuwamo katika Sheria ya Magazeti ya Mwaka 1976.

Vilevile, kuwekwa kwa Vipengele vya Haki za Msingi na Wajibu wa Mwanadamu (Bill of Rights) katika Katiba ya nchi yetu kulibadilisha sheria zote ambazo zinakiuka haki za binadamu. Vifungu vyote tulivyovitaja hapo juu viliguswa moja kwa moja na Vipengele vya Haki za Msingi na Wajibu wa Mwanadamu. Ibara ya 14 ya Katiba inalinda haki ya kuishi na inaitaka jamii kutoa hifadhi ya maisha kwa kila mtu. Kana kwamba hiyo haitoshi, Ibara ya 26(1) na (2) zinataka kila mtu na serikali kutii Katiba ya nchi na vilevile kuchukua hatua za kuheshimiwa haki na sheria za nchi.

Waziri mkuu anayajua haya vizuri. Anafahamu kuwa sheria iliyotumiwa kufungia gazeti, ni sheria katili na imepitwa na wakati. Kuitumia sheria hii kunaendeleza dhana ya kuwa serikali hii inatumia udhaifu wa Katiba na baadhi ya sheria kukandamiza Haki za Binadamu na Uhuru wa Habari! Mambo haya hayakubaliki.

Kutokana na hali hiyo, sisi watetezi wa haki za binadamu na asasi nyingine za kiraia:
1. Tunarejea wito wetu wa kuitaka serikali kulifungulia mara moja na bila masharti, gazeti hili ambalo limekuwa kipenzi cha wananchi. Tunaitaka serikali ndani ya siku saba (7) kutekeleza hilo kwa kuangalia maslahi mapana ya jamii badala ya kuangalia maslahi ya baadhi ya viongozi wenye maslahi fulani katika kutimiza malengo yao binafsi.

Serikali itekeleze takwa hili haraka iwezekanavyo, na kwamba asasi za kijamii hazikubaliani na kauli ya Waziri Mkuu ya kutaka wahusika waende kwenye vyombo vya juu kwa sababu tatu zifuatazo:

Kwanza, sheria ya magazeti hairuhusu ukataji wa rufaa kwa waziri wa Habari ambaye ndiye aliyetuhumu na kuhukumu gazeti bila kutoa nafasi kwa wahusika kusikilizwa. Pili, Waziri Mkuu Pinda pamoja na sheria hiyo kutomtaja, hakueleza kuwa yuko tayari kupokea malalamiko ya MwanaHALISI. Hivyo kutoelekeza kwake tunakuchukulia kama njia ya kukwepa wajibu wake.

Tatu, hatukubaliani na kauli ya Waziri Mkuu na wengine wanaoitaka MwanaHALISI waende mahakamani kutafuta haki yao kwa kuwa serikali yenyewe haikutumia njia ya mahakama kufungia gazeti. Serikali inataka kuitumia mahakama ili kuchelewesha MwanaHALISI kupata haki yake. Nyote mnajua jinsi mahakama zetu zinavyokabiliwa na gonjwa kubwa la ucheleweshaji wa kesi.

2. Serikali, baadala ya kushughulika na watetezi wa haki na wanahabari wanaofichua uovu, ishughulike na wahalifu waliomteka, kumtesa na hatimaye kumtelekeza Dk. Ulimboka. Ushahidi uliobainishwa na gazeti hili haukuacha shaka yeyote juu ya waliohusika na sakata hili, na kama serikali au watendaji wake waliotajwa (na waliohusishwa) wana mashaka wangetumia ushahidi na taarifa zile kutafuta haki zao: kwanini wasiende mahakamani au wajitokeze na ushahidi wa kukanusha yaliyobainishwa?

3. Serikali iachane kabisa na ukandamizaji huu wa haki na uhuru wa habari. Matendo aliyofanyiwa Ulimboka, habari zilizobainishwa na MwanaHALISI juu ya sakata hili na kufungiwa kwa gazeti hili kunaonesha mtiririko wa matukio ya serikali kuminya uhuru na haki.

Ikumbukwe pia kuwa, Kesi Na. 34/2009 iliyofunguliwa tangu 2009 kupinga sheria ya magazeti ya mwaka 1976 iliyotumika kuwafungia MwanaHALISI haijasikilizwa mpaka sasa. Hii inaenda sambamba na serikali kufumbia macho mahitaji ya sheria ya uhuru wa habari na kudharau mapendekezo ya muswada wa habari tangu 2007 bila kupeleka Bungeni.

Kwa hoja hizo, sisi watetezi wa haki za binadamu, asasi za kijamii na wadau wakuu wa habari nchini, tunaendelea kusisitiza kuwa serikali itimize wajibu wake kwa kulifungulia mara moja gazeti hili na kufanyia kazi yaliyobainishwa. Kama ikishindwa kufanya hivyo, tutaitisha maandamano ya kupinga hatua ya serikali kufungia gazeti hili, kuminya uhuru wa habari, haki za binadamu na uteswaji wa wanaharakati na watetezi wa haki na kwamba tukifika hapo tunawaomba waandishi wa habari mtuunge mkono kwa yafuatayo.

i. Msichapishe habari yoyote inayomhusu Waziri wa Habari, Naibu Waziri, Katibu Mkuu wa wizara hiyo, na pia Mkurugenzi wa Maelezo. Tunawasihi wahariri wasiwatume waandishi katika Ukumbi wa Habari Maelezo kwa ajili ya kuchukua habari kama ilivyo kawaida na badala yake Watanzania wote wahakikishiwe kupata habari kwa njia nyingine mbadala.
ii. Tunawasihi wadau wote wanaoweza kutuunga mkono mara tutakapohitaji msaada wao ikiwa ni pamoja na kushiriki kwenye maandamano na kupata mawakili ambao watasaidia katika uendeshaji wa shauri letu mahakamani.
iii. Tunawasihi wanaharakati wote wasichoke wala wasirudi nyuma katika azma hii ya kutetea haki, uhuru na ulinzi kwa haki na watetezi wake.

Marcossy Albanie
Mwenyekiti wa Kamatifor
Asasi ambazo zimetoa tamko la kutaka serikali ifungulie MwanaHALISI ni MISA, Legal and Human Centre, Tanzania Human Rights Defenders Coalition, Human Rights National Association of Educators For World Peace and Citizen Rights Watch.
mwisho


Ndimara TegambwageInformation and Media ConsultantP.O. Box 71775, Dar es SalaamTel: 255 (0)713614872e-mail: ndimara@yahoo.comwww.ndimara.blogspot.com

Sunday, August 19, 2012

Sikukuu ya IDD EL FITR KITAIFA Songea 2012

Habari za Idd el Fitri katika Picha, Picha zote na Juma Nyumayo wa www.ruvumapress.blogspot.com













































Picha Na 4: Mgeni Rasmi wa Idd el fitr kitaifa Mkoani Ruvuma, Said Thabit Mwambungu (Katikati) ambaye ni Mkuu wa Mkoa huo akipokelewa na viongozi wa Msikiti Mkuu wa mkoa wa Ruvuma uliopo Manispaa ya songea

Picha Na3: Mufti wa Tanzania, Sheikh Issa Shaaban Simba akiingia ndani ya Msikiti wa Mkoa wa Ruvuma Manispaa ya Songea kuhudhuria ibada ya Idd el fitr kitaifa nyuma yake akifuatiwa na Mkuu wa mkoa wa Ruvuma Said Thabit Mwambungu

Picha Na 2: Immam wa Msikiti wa Mkoa wa Ruvuma Manispaa ya Songea, Shekh Shaaban Mbaya akitoa hotuba ya Idd el fitr kitaifa mkoani Ruvuma wakati waumin wakimsikiliza

Picha Na1: Baadhi ya waumin wanawake wakiwa wamesimama nje ya msikiti mara baada ya kumaliza swala ya Eid el Fitr kitaifa mkoani Ruvuma.

Sikukuu ya Eid El Fitr kitaifa Songea - Ruvuma

HALI YA HEWA imebadilika hapa Songea, ni manyunyu ya Mvua yanayoambatana na baridi, hali ya utulivu, waumini wa kiislamu na wakikristu wakipishana kwenye mitaaa kadhaa hapa mjini Songea wakielekea kwenye nyumba za Ibada katika siku hii ya leo ya kumaliza Mwezi mtukufu wa mfungo wa Ramadhani 2012.
Watoto wadogo wakiwa wameshikwa mikono na walezi wao bado pia tunakumbuka, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Mrisho Kikwete kumshika mkono Rais wa Malawi Joyce Banda mwishoni mwa mfungo wa Mwezi huu wa Mfungo na kuwahakikishi wananchi wa nchi hizo mbili kuwa hapatakuwa na vita ya kugombea mipaka.
Hapa Songea umetolewa wito kwa waislamu wote nchini kuhakikisha kuwa wanauendeleza uadilifu na mafundisho ya dini hiyo ili kudumisha amani na usalama wa watanzania na majirani zao hpa duniani.

Maombi hayo yalikuwa ni sehemu ya Ibada ya swala ya Idd el fitr ilyofanyika katika Msikiti wa mkoa wa Ruvuma uliopo mjini Songea iliyohudhuriwa na maelfu ya waumini wa Dini hiyo wakiongozwa na mufti wa Tanzania Sheikh Issa Shaaban Simba na Mgeni Rasmi kitaifa Mkuu wa mkoa wa Ruvuma Said Thabit Mwambunga.

Immam wa Msikiti huo, Sheikh Shaaban Mbaya katika maombi maalum ya kuliombea taifa na viongozi wake wapate afya njema na uwezo wa kuwatumikia watanzania ili wawe na amani, alisema kuwa waumini wa kiislamu hawatakiwi hata kidogo kumbagua muislam au asiye kuwa muislam katika maisha yao ya kila siku.

Alisema, mafundisho ya dini hiyo yana sisitiza upendo na amani ili kuenzi uumbaji wa mwenyezi Mungu, ambaye ni mwingi wa rehema na kwamba viumbe vyote vya ardhi, majini na hewani ameviumba yeye mwenyewe bila ubaguzi kwa manufaa ya viumbe kwakuwa vinategemeana.

Alieleza zaidi kuwa waumini hao wafuate mafunzo toka kiongozi wao, Mtume Muhammad (SAW) ambaye aliweza kuwatunza mayatima na watu wasiokuwa na uwezo kiuchumi ambao wasiowaislamu na waislamu ili wapate furaha ya maisha yao ya kila siku licha ya shida na upweke waliokuwa nao.

"Ndugu waumin haina maana wakati huu wa sikukuuu mkajipamba kwa nguo safi na mkala vyakula vizuri wakati mioyo yenu na matendo yenu hayampendezi mwenyezi mungu," alisema Immam Sheikh Shaaban Mbaya na kusisitiza kuwa ni vyema wakaona umuhimu wa kuendeleza mafundisho waliyoyapata mwezi Mtukufu wa ramadhani kwa manufaa ya watu wote.

Aidha, Sheikh Mbaya alisema, Uchoyo na tamaa za mali, matendo mabaya na uroho wa madaraka na kudhalilisha wengine ndiyo chanzo cha kuvuruga amani iliyopo kuanzia ngazi ya familia, kijiji wilaya taifa na kimataifa.

Saturday, August 18, 2012

TANZIA

TANZIA - MWANDISHI MBOGORA AFARIKI DUNIA
Wakuu,
Habari za leo, habari za Jumamosi,
Tumepata taarifa kutoka Baraza la Habari Tanzania (MCT) kwamba mmoja wa maofisa wake na Mwanahabari na Mhariri wa siku nyingi, Alfred Mbogora amefariki Dunia leo saa 11.00 alfajiri katika hosipitali ya Taifa ya Muhimbili.
Katibu Mtendaji wa MCT, Kajumbi Mukajanga amesema kwamba Mbogora alilazwa Muhimbili tangu Jumanne baada ya kuwa ameanguka katika eneo la Tegeta, mara baada ya kupata chakula wakiwa njiani kwenda Bagamoyo kwa shughuli za kikazi.
Kabla ya kuanguka, Mbogora alikuwa akilalamika kwamba anasikia kuishiwa nguvu kwenye mguu na mkono na alipojaribu kusimama ili kutembea kutokana na hali aliyokuwa akiisikia mwilini alianguka.
Tangu wakati huo (baada ya kuanguka) alikata kauli na hakuwa kusema chochote hadi hapo alipokata roho leo alfajiri. Ni pigo kwa sekta ya habari nchini, kumpoteza mwanahabari mwenzetu ambaye ametoa mchango mkubwa katika sekta yetu ya habari.
Inasadikiwa kwamba msiba wa Mbogora uko nyumbani kwake Segerea, lakini taarifa zaidi tutazipata kadri tutakavyoendelea kuwasiliana na MCT pamoja na familia ya marehemu.
Tunachukua fursa hii kuwapa pole wafiwa wote, kwanza ni familia ya marehemu, MCT na wanahabari wote nchini. Bwana alitoa na Bwana ametwaa jina lake luhimidiwe, Amen.--
Neville C. Meena,
Secretary General,
Tanzania Editors Forum - TEF,
Dar es Salaam - Tanzania.
Cell: +255 - 787 - 675555
+255 - 753 - 555556

Thursday, August 16, 2012

Maandalizi ya Sensa, Cheki Bango

KILA  MMOJA  WETU ANAPASWA  KUSHIRIKI  SENSA AGOST 26Sensa kwa maendeleo, hivi sasa nchini Tanzania wimbo ni mmoja tu. Sensa kwa Maendeleo, Jiandae Kuhesabiwa.

Majimaji yajengewa uzio

Kaimu Muhifadhi Kiongozi wa Makumbusho ya Taifa ya Mashujaa wa Majimaji Songea, Balthazar Nyamusya (Kulia) akimkaribisha Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Said Thabit Mwambungu alipotembelea makumbusho hayo kwa maraq ya kwanza tangu ateuliwe kuwa mkuu wa Mkoa huo, nyuma ya Mwambungu ni Chief wa wangoni,  Emmanuel Xavery Zulu Gama.
Makumbusho haya sasa yanajengewa uzio, yanapendeza kwelikweli. Hongera Shirika la Makumbusho ya taifa kwa kazi nzuri inayosimamiwa na Bw. Balthazar Nyamusya hapa Songea.