Saturday, July 30, 2011

Breaking Neeewws! Mstahiki Meya wa Manispaaya Songea, Ali Said Manya

Mstahiki Meya wa Manispaa ya Songea Mheshimiwa Diwani wa Lizaboni, Ali saidi Manya, amefariki dunia leo katika Hospitali ya Misheni Peramiho, Maili 15 toka Songea mjini. Taarifa za kifo chake zilizopokelewa kwa mshtuko mkubwa na wananchi mkoani hapa, zimetangazwa na Naibu Meya wa Manispaa ya Songea, Mheshimiwa Mariam Dizumba. Mstahiki Meya Ali said Manya wakati wa uhai wake pichani kushoto mwenye Suti nyeupe akifurahia jambo alilosema Mwenyekiti wa Ruvuma Press Club Juma Nyumayo, (aliyesimama) alipohudhuria kikao cha wadau wa habari mkoani Ruvuma mapema mwaka huu. Kwa mujibu wa Naibu Meya Mazishi yake yatafanywa Jumatatu, Nyumbani kwake Lizaboni Manispaa ya Songea kwa heshima zote za chama chake chja mapinduzi na serikali ya manispaa ya Songea.




Wednesday, July 20, 2011

Miaka 50 baada ya Uhuru, mafiga matatu yatumika kusonga ugali

Mambo ya lishe, bado mika 50 baada ya Uhuru mwanamke huyu anawakilisha kundi kubwa la wanawake nchini Tanzania kupika kwa kutumia mafiga matatu na kutumia nishati ya kuni nyingi kama ilivyokuwa enzi ya Adam na Hawa, kwa hali hii ukombozi wa kimapinduzi na haki za uchumi kuwafikia wanawake walio pembezoni bado ni changamoto kubwa.
Mwezeshaji Neema Duma Toka TGNP Dar es Salaam, akiwawezesha Madiwani wanawake viti maalum Mkoa wa Ruvuma katika Ukumbi wa CWT mkoawa Ruvuma mjini Songea kuhusu kampeni ya haki za kiuchumi kwa wanawake walio pembezoni. Changamoto kubwa waliyonayo madiwani hao ni kutothaminiwa na madiwani wa Kata zao na baadhi ya wataalamu kwenye halmashauri zao. Picha na Maelezo yote na Juma Nyumayo.
Mika

Tuesday, July 19, 2011

Mfumo Dume bwana,, wilaya ya Namtumbo kiboko!

HAPA NI BAADHI YA WANAWAKE WALIOTELEKEZWA NAMTUMBO WAKIWA NA WATOTO WAO KAMA WALIVYOKUTWA NA KAMERA YETU.


Wanaume watelekeza familia, kukwepa majukumu

Na Juma Nyumayo, Namtumbo.

UMEZUKA mtindo wa wanaume hasa vijana kuwakimbia wasichana waliowapatia ujauzito na kutelekeza familia kuwaweka wanawake na watoto katika hali ngumu kimaisha wilayani Namtumbo mkoa wa Ruvuma.

Wasichana na akina mama waliohojiwa na mwandishi wa habari hii wamekili kutelekezwa na kuamua kuishi kwa wazazi walikotoka baada ya vijana hao kuwakimbia wakiwa wajawazito na wengine wakiwa wamejifungua na kuwaachia majukumu yote ya kugharimia matunzo ya mamba na hatimaye watoto.

Mmoja wa aliyekimbiwa akiwa na ujauzito na sasa amejifungua, Blandina Mbawala (17) alisema anapata shida na mtoto wake hasa akipata homa wakati wa usiku, kwani hivi sasa huduma zote zinatolewa na dada yake Donatha Mbawala ambaye naye analea kachanga ka mwezi mmoja na katorokwa na mumewe.

“Huyo Bwana kanikimbia, naishi na dada yangu anayenisaidia kulea mwanangu,” alisema Blandina ambaye bado hana ujuzi wa malezi kulingana na umri wake mdogo.

Akizungumzia tatizo hilo ambalo linaweza kusababisha kuporomoka kwa ustawi wa familia wilayani Namtumbo, Rashidi Tuppa mkazi wa Mjini Namtumbo alisema vijana wengi wilayani hapo wanamtindo wa kukwepa majukumu ya kutunza familia na kuwaachia wazazi wao au wanawake.

“Vijana wengi wa kiume wanaotelekeza familia hawapendi kufanya kazi ili wajikimu kimaisha, na hivyo kukwepa majukumu ya kuhudumia wachumba waliowapatia ujauzito au watoto,” alisisitiza Tuppa.

Fairuna Runje mkazi w Minazini Namtumbo anailalamikia tabia hiyo si kwa vijana wa kiume tu bali kwa wanaume watu wazima pia wana mtindo huo wa kukwepa majukumu ya kazi na kungojea kuhudumiwa na wake zao.

“Hawa wanaume waliotuoa ni kama njiwa wanasubiri kulishwa kwenye tundu, hawafanyi kazi kazi ya kuoa wanawake wawili hadi watano ili tushindane kuwahudumia,” alisema Fairuna.

Mkuu wa wilaya ya Namtumbo, Saveri Maketta, amekili kuwa licha ya mfumo dume unowakabili wakazi wa wilaya hiyo wa kuwakandamiza wanawake katika shughuli za uzalishaji mali na malezi bado wananchi wa wilaya hiyo wanahitaji elimu ya uamsho wa usawa wa kijinsia ili kuleta maendeleo na maisha bora kwa kila mwana Namtumbo.

“Mfumo dume ni tatizo kubwa wialayani kwangu na hivi mwanamke anabebeshwa kila shughuli wakati wanaume hutumbua maisha,” alisema Maketta.

Alisema hivi sasa katika kila kikao anachohutubia anawaeleza madhara ya mfumo dume katika kuchachamua maendeleo ya wakazi wa wilaya hiyo.

Mwisho.

Wasichana 50 kurejeshwa nchini toka Msumbiji


Usafirishaji binadamu kutumikishwa nje kukomeshwa

Na Juma Nyumayo, Songea

SERIKALI mkoani Ruvuma imepania kukomesha kabisa biashara ya usafirishaji binaadamuna kuhakikisha inawarejesha wasichana wapatao 50 waliosafirishwa kinyume na sheria kwenda nchini Msumbiji kwa ushirikiano na vyombo vya usalama vya nchi hiyo jirani.

Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Ruvuma Michael Kamuhanda, alisema hilo alipohojiwa na Mwaandishi wa habari hii ambaye ni mwanachama wa mtandao wa kufuatilia masuala ya usawa wa Jinsia mikoa ya Nyanda za Juu Kusini.

Kamanda Kamuhanda, alisema hivi sasa wanahabari za kiintelijensia ambazo zitatumika kuwakamata wote waliopo kwenye mtandao huo hapa nchini na wale wanaoshirikiana nao Nchini Msumbiji kufanya biashara hiyo haramu inayodhalilisha utu.

“Tutatumia sheria ya kupinga biashara ya kusafirisha binaadamu, Sheria ya kutumikisha watoto na kwakuwa Tanzania na Msumbijji tunashirikiana kupitia Interpol na Ujirani mwema tulionao tutakomesha biashara hii,” alisema kamanda Kamuhanda.

Inasadikiwa kuna zaidi ya wasichana nje ya shule na wanafunzi wa shule za msingi na sekondari zaidi ya 50 waliosafirishwa kwenda maeneo ya Machimbo nchini Msumbiji kufanyishwa kazi za ukhaba katika madangulo na wakati mwingine kuchukuliwa picha za uchi.

Hata hivyo Kamanda Kamuhanda aliziomba taasisi mbalimbali wakiwemo, watu binafsi na Mtandao wa Jinsia nchini (TGNP) kushiriki kutoa elimu kwa wazazi na walezi wa watoto hao madhara ya kukubali kuwakabidhi watu kwa ulaghai wa kupata mshahara mnono huko nchi jirani jambo ambalo amethibitisha kuwa ni vigumu kupatikana.

“Kule hakuna mshahara ni mateso matupu, na tukibaini mzazi au mlezi ameshiriki tutamchukulia hatua za sheria,” alisema Kamuhanda.

Wakati huohuo, Mkuu wa wilaya ya Namtumbo Saveri Maketta amechukua hatua ya kuwaelimisha watu waishio mpakani kandokando ya mto Ruvuma kuhakikisha wanatoa taarifa kwa vyombo vya dola au maafisa watendaji pale watakapoona wasichana wanavushwa ng’ambo ya Msumbiji kwa lengo la kwenda kufanya kazi zisizojulikana.

“Tumewaambia huyo mwajiri awe mwafrka au mzungu lazima serikali yetu ifahamu, na kwamba Kivuko cha Magazini kinaimarishwa kuzuia usafirishaji wa binadamu,” alisema Maketta.

Hivi karibuni Jeshi la Polisi mkoani Ruvuma likishirikiana na polisi wa Msumbiji waliwarejesha wasichana wanafunzi wa sekondari wawili waliosafirishwa kinyume na sheria kwenda machimbo ya Tulo nchini Msumbiji.

Mwisho.